Mil 754.6/- zatumika kuboresha malazi Rubondo

SERIKALI kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imetumia sh milioni 754.60 kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya malazi ya watalii katika Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo.

Mradi huo unaolenga kuboresha huduma ya malazi unahusisha ujenzi wa malazi ya watu mashuhuri, ujenzi wa nyumba 03 za kulaza watalii wa hadhi ya juu kila moja vyumba viwili na jengo la kusubiria watu mashuhuri.

Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo, Dk Imani Kikoti.

Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Rubondo, Dk Imani Kikoti ametoa taarifa hiyo katika mahojiano maalum na waandishi wa habari waliotembelea mradi huo uliofika zaidi ya asilimia 80 ya utekelezaji.

SOMA: TANAPA kufadhili vizimba vya samaki kudhibiti uvuvi haramu Ziwa Victoria

Dk Kikoti amesema hatua hiyo inalenga kukidhi mahitaji ya idadi ya watalii wanaozidi kuongezeka kisiwani humo ambapo kwa sasa kuna wastani wa watalii 5,000 kwa mwaka na lengo likiwa kufikia watalii 10,000.

Amesema kukamilika kwa huduma ya malazi ya kisasa inatarajia kukifanya kisiwa cha Rubondo kuwa moja ya hifadhi inayopokea idadi kubwa ya watalii na kuiongezea mapato serikali kupitia sekta ya utalii.

Kwa mujibu wa Dk Kikoti hadi mwaka wa fedha 2024/25 Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) linakusanya wastani wa sh milioni 700 kwa mwaka kutoka kisiwa cha Rubondo lakini lengo ni kufikia sh bilioni moja kila mwaka.

“Majengo haya ni ya kisasa ambayo yanaweza kuhudumia watalii wa ndani lakini pia hata watalii wa nje, majengo haya yalianza kujengwa mwaka 2023 na yanatarajiwa kukamilika mwaka huu 2025”, amesema.

Ofisa Uhusiano kutoka TANAPA, Catherine Mbena.

Ofisa Uhusiano wa TANAPA, Catherine Mbena amesema shirika hilo limekuja na mpango mkakati wa kuboresha huduma za malazi na miundombinu kwenye hifadhi zote ili kukuza sekta ya utalii nchini.

Amesema maboresho hayo yanaenda sambamba na juhudi za kutangaza utalii zinazofanyika ili kuhakikisha kuwa maendeleo ya sekta ya utalii yanajibu na kuaksi uhalisia wa ubora miundombinu ya utalii nchini.

“Wageni wanapokuja shughuli za kufanya ni nyingi, sasa usipokuwa na miundombinu ya malazi maana yake hawawezi wakakaa kwa muda unaotosha kukamilisha furaha yao na kufanya shughuli nyingine”.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button