Dk Mpango: Tulinde amani kumuenzi Nyerere

MAKAMU wa Rais, Dk Philip Mpango amesema ni muhimu Watanzania walinde amani kumuenzi Baba wa Taifa, Julius Nyerere.
Dk Mpango amesema hayo kwenye kilele cha mbio za Mwenge wa Uhuru na kumbukizi ya miaka 26 ya kifo cha Baba wa Taifa, Julius Nyerere kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.
Amesema Nyerere aliacha misingi mikuu minne ukiwemo wa kulinda amani, uhuru wa taifa, kudumisha umoja na kusimamia haki miongoni mwa jamii.

Dk Mpango alitaja msingi wa pili ni kujenga na kuimarisha maadili mema ndani katika nchi hasa miongoni mwa vijana ambao ndio taifa la sasa na baadaye.
Amesema ni muhimu Watanzania wakemee mmomonyoko wa maadili ikiwemo rushwa na ufisadi ambavyo Baba wa Taifa alivichukia sana na kuvipiga vita kwa vitendo.
SOMA: JULIUS KAMBARAGE NYERERE: Shina la amani na ukombozi
“Jambo la tatu ni kuwajibika kwa kila mwananchi kufanya kazi kwa bidii ili kuboresha maisha na kuinua vipato vyetu hivyo kuchangia katika ujenzi wa taifa,” ameeleza Dk Mpango.
Vilevile, Dk Mpango amewahimiza vijana kuchangamkia fursa zilizopo na zinazochipukia katika sekta mbalimbali kama vile kilimo, biashara, ujasiriamali, Tehama, sanaa na utamaduni.
Ameongeza kuwa kila Mtanzania lazima atambue kuwa anao wajibu wa kujenga nchi kwani Tanzania itajengwa na
Watanzania wenyewe.
Dk Mpango alitaja jambo la nne kuwa ni utunzaji na uhifadhi wa mazingira hususani katika kulinda vyanzo vya maji, upandaji wa miti na kufanya usafi wa mazingira mambo ambayo Mwalimu Nyerere alikuwa mfano bora wa kuigwa.
Sambamba na hayo, Dk Mpango alimwelezea Baba wa Taifa kama mtu wa mfano ambaye kila Mtanzania anapaswa kumuiga hususani katika kujenga umoja wa kitaifa ili kuunda taifa imara.

Pia, amesema Watanzania wanapaswa kuwa wazalendo wa nchi yao pamoja na kuweka usawa, haki na kuzingatia matakwa ya wengi katika maamuzi.
Amesema juhudi za Mwalimu Nyerere zililisaidia taifa kupata Uhuru mwaka 1961 na kumtaja kama Mwanamajumui wa kweli wa Afrika aliyeonesha uzalendo mkubwa kwa bara hilo.
Ameongeza Mwenge wa Uhuru ulipoasisiwa ulilenga kuidhihirishia dunia na kuonesha mfano kwa mataifa yaliyoendelea kuwa chini ya udhalimu wa kikoloni maana ya taifa huru na uwezo wake wa kujitawala pasipo kuingiliwa na mtu yeyote.
“Maono hayo ya Mwalimu Nyerere yalikuwa sahihi na hasa kwa taifa lililokuwa ndio kwanza linajinasua kutoka katika makucha ya wakoloni aliposema ‘Sisi tumekwisha uwasha Mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro umulike nje ya mipaka yetu ulete matumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali penye chuki na heshima palipojaa dharau,” amesema Dk Mpango.
Amesema falsafa hiyo ya Nyerere imekuwa dira ya mbio za Mwenge kwa miaka yote ikiendeleza dhamira ya kuhamasisha uzalendo na ujasiri wa kupambana na maovu katika jamii na kuleta amani, upendo, maendeleo na mshikamano katika taifa.
Amesema kupitia falsafa hiyo nchi imefanikiwa katika mambo mengi ikiwemo kuondoa ubaguzi, ukabila na kujenga umoja wa kitaifa, kuimarisha utawala bora, kupinga dhuluma, dharau, chuki na kupambana na ufisadi na rushwa.
Dk Mpango ameweka wazi kuwa serikali itaendelea kuienzi falsafa hiyo kwa maendeleo ya taifa.
Amethibitisha kuwa mbio za Mwenge mwaka huu zimejielekeza mahususi kuhamasisha wananchi kushiriki katika uchaguzi mkuu na hivyo kuwaomba Watanzania wote waliojiandikisha kujitokeza kwa wingi kwenye kampeni ili kusikiliza sera na kujitokeza kwa wingi kupiga kura siku ya uchaguzi kuchagua viongozi bora.
“Nawasihi Watanzania wenzangu kufuata wito wa Baba wa Taifa aliyewataka kuchagua viongozi ambao watakidhi matarajio ya Watanzani ana kuleta mabadiliko,” ameongeza Dk Mpango.
Kuhusu maadhimisho ya wiki ya vijana, Dk Mpango amesema serikali imeendelea kuadhimisha Wiki ya Vijana Kitaifa ili kutambua mchango wao katika ujenzi wa taifa.
Amesema kupitia maonesho ya wiki ya vijana yaliyofanyika Mbeya, vijana wameonesha uwezo mkubwa katika ujasiriamali na matumizi ya teknolojia katika sekta mbalimbali za maendeleo.
Amezitaka wizara zinazohusika na maendeleo ya vijana Bara na Visiwani, kuratibu vyema sera za maendeleo ya vijana na kuhakikisha sekta zote zinatekeleza ajenda ya kukuza ushiriki wa vijana katika shughuli za maendeleo.
Tukio hilo pia lilienda sambamba na uzinduzi wa Kitabu cha Miaka 60 ya Mbio za Mwenge wa Uhuru Tanzania akisema kimeandikwa ili kuhifadhi kumbukumbu na chimbuko la mbio hizo nchini.
Amesema kitabu hicho ni urithi na rejea muhimu kwani kinakumbusha kuwa haki, usawa, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa uliopo, msingi wake ulijengwa na waasisi wa taifa kupitia Mwenge wa Uhuru.



