Waandishi wapewa nguvu kukemea ukatili mtandaoni

SHIRIKA la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF Tanzania) kwa kushirikiana na GIZ limeendesha kambi maalum ya mafunzo kwa waandishi wa habari kwa muda wa siku tatu, ikiwa ni maandalizi kuelekea Kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia mwaka 2025.

Mafunzo hayo yamelenga kuunga mkono juhudi za kitaifa kupitia Mdahalo wa Kitaifa kuhusu Ukatili wa Kidigital na Ukatili Dhidi ya Wanawake katika Uchaguzi, ikiwa ni hatua ya kuimarisha ushiriki salama wa wanawake katika nyanja za kisiasa na kijamii.

Kambi hiyo imewaleta pamoja waandishi wa habari na wataalamu wa mawasiliano kutoka taasisi mbalimbali, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika maeneo ya uhusiano kwa umma, maadili ya uandishi, usalama wa kidijitali na usimulizi wa habari unaozingatia usawa wa kijinsia na haki za binadamu.

Mkurugenzi wa WiLDAF Tanzania, Wakili Anna Kulaya, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada endelevu za kujenga mtandao wa wanahabari wanaochochea mabadiliko ya kijamii kupitia uandishi wa habari unaolinda hadhi, haki na usawa wa kijinsia.

“Tunataka kuona waandishi wa habari wanakuwa mstari wa mbele katika kupaza sauti za wanawake na wasichana, kupinga ukatili wa aina zote, na kutumia teknolojia kwa njia salama na chanya,” alisema Wakili Kulaya.

Kwa upande wake, mwakilishi wa GIZ alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za maendeleo na vyombo vya habari katika kupambana na ukatili unaochochewa na teknolojia, hasa ule unaowalenga wanawake katika siasa na uchaguzi.

“Kuhakikisha sauti za wanawake zinasikika bila hofu ni msingi wa demokrasia. Kupitia mafunzo haya, tunajenga kizazi cha waandishi wa habari wanaotetea haki, usawa na uwajibikaji wa kijamii,” alisema mwakilishi huyo. SOMA: Gwajima: Pato la taifa linateketea kupambana na ukatili

Kambi hiyo pia ni sehemu ya maandalizi ya Mdahalo wa Kitaifa kuhusu Ukatili Unaotokana na Teknolojia, utakaowakutanisha wadau kutoka serikalini, asasi za kiraia, vyombo vya habari na washirika wa maendeleo, kujadili mikakati ya pamoja ya kukomesha ukatili wa kijinsia mtandaoni na nje ya mtandao.

WiLDAF Tanzania na GIZ wamesisitiza dhamira yao ya kuendelea kuwekeza katika elimu, uhamasishaji na ubunifu wa kimawasiliano ili kukuza jamii yenye usawa wa kijinsia na heshima kwa haki za binadamu.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button