Serikali ya NLD yaahidi mikopo bila riba

MGOMBEA urais kupitia chama cha National League for Democracy (NLD), Doyo Hassan Doyo amesema serikali ya chama hicho itatoa mikopo isiyo na riba kwa wafanyabiashara.
Doyo alitoa ahadi hiyo alipofanya ziara kutembelea masoko jijini Tanga juzi na akasema watafanya hivyo ili wafanyabiashara wawe na mitaji isiyo na matatizo.
Alisema watahakikisha wafanyabiashara wanapata mikopo yenye heshima ambayo itatolewa na halmashauri jambo ambalo linawaondolea mzigo ukiwemo msongo wa mawazo kutokana na madeni ya mikopo ya kausha damu.
Doyo alisema serikali ya chama hicho itajenga soko la ghorofa tatu ili kulipa hadhi soko hilo kongwe liwe la kisasa ili waweze kufanya biashara za bila changamoto zilizopo kwa sasa.
Alisema katika ujenzi wa soko hilo, eneo la chini litakuwa la mbogamboga na katikati watu wa mchele na nafaka juu na watu wa nyanya na mambo mengine mtu akifika sokoni amalize kila kitu.
“Sokoni si sehemu ya kuuza tu mbogamboga na nyanya bali ni sehemu ya biashara zote. Mkinichagua, tutakwenda kujenga soko la biashara na nyie muwe watu kwa watu kwa kuwa kwenye soko lenye hadhi na meza za kisasa,” alisema Doyo.
Alimuombea kura mgombea ubunge wa Jimbo la Tanga kupitia NLD, Ramadhani Mwaligo ili akichaguliwa ashirikiane nae kuwaletea maendeleo kwa wananchi.



