Ethiopia Yaingia BRICS

ETHIOPIA imefanikiwa kuwa mwanachama wa jumuia ya BRICS, hatua itakayoiweka nchi hiyo kwenye jukwaa la kimataifa na kuipa nafasi ya kusisitiza masuala muhimu ya bara la Afrika na masuala yake ya maendeleo endelevu.
Hatua hii inakuja baada ya nchi zaidi ya 40 kuonyesha nia ya kujiunga, huku Ethiopia ikichaguliwa miongoni mwa nchi sita zilizokubaliwa katika Mkutano wa Johannesburg.Kawaida, Ethiopia imejulikana kwa sera yake isiyoegemea upande wowote na kuunga mkono harakati za ukombozi barani Afrika.
Kujiunga na BRICS kunatoa fursa ya kushirikiana na nguvu kubwa za kimataifa kama China na Urusi, pamoja na kufungua milango ya kujenga uhusiano na eneo la Mashariki ya Kati na Kaskazini mwa Afrika (MENA). Ushirikiano na nchi za MENA umekuwa na changamoto kwa Ethiopia kutokana na migongano ya kihistoria, ikiwa ni pamoja na mgogoro wa GERD, ambapo nchi za eneo hilo zilikosoa mara kadhaa hatua za Ethiopia.
Kujiunga na BRICS kunaiwezesha Ethiopia kupata jukwaa la kimataifa la kueleza maslahi yake na kushirikiana kwa uwiano na nchi za MENA. Kipengele kingine cha muhimu ni kijiografia; Ethiopia ipo katika Pembe ya Afrika, karibu na Bahari Nyekundu, hali inayoiwezesha kuwa daraja kati ya Afrika ya Kusini mwa Jangwa na dunia ya Kiarabu.
Hii itarahisisha ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kidiplomasia na nchi za MENA, ikiwemo kushirikiana katika masuala ya mafuta, biashara na usalama wa kikanda. SOMA: Dhahabu na BRICS: Njia mpya ya Tz kulinda uhuru wa kifedha
Wataalamu wa siasa za kimataifa wanasema kuwa, ili kufanikisha nafasi yake, Ethiopia inapaswa kuwa makini katika kushirikiana na wanachama wapya wa BRICS, huku ikihakikisha inaendelea kushirikiana na mashirika ya kikanda ya MENA kwa njia yenye uwiano na utulivu. Hatua hii inatabirika kuongeza sauti ya Ethiopia katika masuala ya kimataifa na kuimarisha uhusiano wake wa kidiplomasia.


