Msajili Hazina apanga kukusanya tril 2/-

OFISI ya Msajili wa Hazina imepanga kukusanya Sh trilioni mbili za gawio la mashirika ya umma kwa mwaka wa fedha 2025- 2026. Hazina imejiwekea kiasi hicho baada ya serikali kuiwekea lengo la kukusanya Sh trilioni 1.7. Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu amesema Dar es Salaam hivi karibuni kwamba ofisi yake imejipanga kuendelea kuimarisha mashirika ya umma ili kuongeza ufanisi katika huduma na uwekezaji.

“Usimamizi bora wa utendaji wa taasisi na mashirika ya umma ni chachu ya mageuzi katika uendeshaji wa sekta hii,” alisema Mchechu Desemba 5, mwaka huu. Alisema uimarishaji wa usimamizi huo utaongeza uzalishaji, kuboresha uchumi na kuongeza mapato ya kodi na yasiyo ya kodi ambayo ni muhimu katika kuwezesha serikali kutekeleza majukumu yake.

Kauli hiyo ya Mchechu imekuja baada ya ziara ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo katika Ofisi za Msajili wa Hazina Dar es Salaam, Desemba 5, mwaka huu. Katika ziara hiyo, Profesa Kitila alitoa onyo la kuzifuta ama kuziunganisha taasisi na mashirika ya umma yasiyoonesha ufanisi endapo hayatachukua hatua madhubuti za kuboresha utendaji wao.

Amesema haiingii akilini kuona baadhi ya mashirika ya umma yakishindwa kutoa gawio stahiki licha ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali. Amesema serikali itatoa muda maalumu kwa taasisi husika kujirekebisha kabla ya kuchukua maamuzi ya kuyaunganisha au kuyafuta itakapobidi. “Ni afadhali kuwa na mashirika machache ya biashara, lakini yanayotoa gawio stahiki kwa serikali,” alisema.

Kwa mujibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina, serikali inamiliki hisa katika taasisi na kampuni 308 na kati ya hizo ni kampuni 91 pekee ndizo zinazofanya biashara na 217 hazifanyi. Kitila alisema serikali inataka kuona wananchi wakifaidi matunda ya uwekezaji wake wa Sh trilioni 92.3 uliofanywa katika mashirika ya umma na kwamba itaongeza ufanisi zaidi kwa kuhakikisha upatikanaji wa watendaji na wajumbe wa bodi za mashirika ya umma unafanyika kwa uwazi na ushindani.

“Kazi yangu ni kuhakikisha tunakuwa na sheria bora ya uwekezaji wa umma itakayo chochea ufanisi wa mashirika ya umma,” alisema.Amesema anaamini maboresho ya muswada huo yatafanyika kwa haraka na hatimaye kusomwa kwa mara ya pili bungeni katika siku za karibuni. SOMA: Ofisi ya msajili wa hazina yaandaa CEO Forum 2025

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button