Azaki Week Kufanyika Arusha Juni 2

DAR-ES-SALAAM: WIKI ya Asasi za Kiraia (Azaki) kwa mwaka 2025 inatarajiwa kufanyika kuanzia Juni 2 hadi 6 mkoani Arusha, kwa mujibu wa taarifa kutoka The Foundation for Civil Society (FCS).
Maadhimisho hayo yanalenga kukutanisha wadau mbalimbali kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kwa ajili ya kutathmini mafanikio ya Azaki na kupanga mikakati ya kuimarisha maendeleo ya taifa kupitia ushirikiano wa kijamii na kiuchumi.
Akizungumza na waandishi wa habari kuelekea maadhimisho hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi, Nesia Mahenge, amesema kuwa tukio hilo litakuwa jukwaa muhimu kwa wadau kubadilishana uzoefu na kujadiliana kuhusu namna bora ya kushirikiana katika kufanikisha maendeleo endelevu.
“Tunashirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo wa serikali, sekta binafsi na washirika wa maendeleo ili kuhakikisha kuwa rasilimali zinazotolewa zinawanufaisha wananchi kwa njia endelevu na shirikishi,” alisema Mahenge.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa FCS, Justice Rutenge, alibainisha kuwa hii ni mara ya saba mfululizo kwa Wiki ya Azaki kufanyika, huku mwaka huu ikiambatana na kaulimbiu isemayo: “Njia gani tunaweza kutumia ili kufikia maendeleo.”
Rutenge alieleza kuwa Azaki zimekuwa na mchango mkubwa katika maandalizi ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050 ambayo tayari imekabidhiwa serikalini na inasubiri kuzinduliwa rasmi.
“Azaki zimekuwa mstari wa mbele katika kuchangia mawazo, kushiriki kikamilifu na kuhakikisha kuwa dira hiyo inaakisi matarajio na mahitaji halisi ya Watanzania,” alisema.
Maadhimisho ya mwaka huu pia yataangazia masuala ya utawala bora, uwajibikaji, utoaji wa huduma bora kwa jamii, ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi, pamoja na maendeleo jumuishi.
Pia kutakuwa na mikutano ya kitaalamu, warsha za kujengeana uwezo, kliniki za maarifa na mijadala ya wazi inayowaleta pamoja wadau kutoka nyanja mbalimbali.
Katika hatua nyingine, Benki ya Stanbic Tanzania imetangaza kudhamini maadhimisho hayo kwa kuchangia shilingi milioni 40. SOMA: Watu 500 kushiriki wiki ya Azaki
Akizungumza kwa niaba ya benki hiyo, Mkuu wa Kitengo cha Taasisi za Umma na Mashirika Binafsi, Doreen Dominic, alisema udhamini huo unaakisi dhamira ya benki hiyo katika kusaidia maendeleo shirikishi.
“Huu ni mwaka wa nne mfululizo tunashirikiana na Azaki, na tunaamini kuwa maendeleo ya kweli yanatokana na mazungumzo ya wazi, ushirikiano na kuaminiana,” alisema Dominic.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tanzania Bora Initiative, Ismail Biro, alisema wiki hiyo itaangazia pia changamoto zinazozikumba Azaki na njia bora za kuzitatua kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, huku makundi maalum kama vijana, wanawake na watu wenye ulemavu yakipewa kipaumbele.
FCS imehimiza washiriki kujisajili mapema ili kuhakikisha wanapata fursa ya kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo ambayo yanatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa wote wenye nia ya dhati ya kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya taifa.