Matinyi aongoza ujumbe wa Tanzania Oslo

BALOZI wa Tanzania nchini Sweden, Mobhare Matinyi aliongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Biashara kati ya nchi za Nordic na Afrika, uliofanyika jijini Oslo, Norway.

Akifungua mkutano huo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Norway, Andreas Motzfeldt Kravik, alisisitiza umuhimu wa nchi za Nordic na Afrika kuwa na sera rafiki za biashara na kuimarisha ushirikiano kati ya sekta za umma na binafsi katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati.  Aliongeza kuwa bara la Afrika linabeba mustakabali wa dunia.

Washiriki wa mkutano huo walitoka sekta binafsi, jumuiya za wafanyabiashara, viongozi wa serikali, wanadiplomasia na mashirika mbalimbali kutoka duniani, ikiwemo Marekani. Kaulimbiu ya mkutano ilijikita katika kuhamasisha biashara, matumizi ya nishati safi, na kuboresha miundombinu kati ya nchi za Nordic na Afrika.

Ujumbe wa Tanzania chini ya Balozi Matinyi ulijumuisha Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Wakulima wa Maua, Matunda na Mbogamboga (TAHA), Jacqueline Mkindi, na ulitumia fursa hiyo kutafuta masoko mapya ya bidhaa za Tanzania, ikiwemo kahawa, chai, korosho, vitunguu, viungo, maua na matunda.

Balozi Matinyi pia alifanya mazungumzo ya awali na kampuni za nishati safi za Norway, ikiwemo: SCATEC iliyo wakilishwa na Afisa Mtendaji Mkuu Terje Pilskog, RENERGY iliyo wakilishwa na Afisa Uendeshaji Mkuu Mikkel Hansen, na CAMBI iliyo wakilishwa na Meneja wa Mauzo wa Kanda ya Afrika, Gary Brown. SOMA: Maadili na haki za binadamu: Mvutano wa aina yake Afrika

Ujumbe wa Tanzania ulijikita pia katika kutafuta fursa za kupunguza utoaji wa hewa ya ukaa na majitaka kwa kuendeleza teknolojia bunifu za nishati safi. Aidha, ulilenga kuendeleza mnyororo wa thamani kwenye sekta ya madini kupitia ujenzi wa miundombinu imara na rafiki kwa wachimbaji wadogo.

 

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button