MDHIBITI na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali imetoa mapendekezo kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuboresha mfumo wa ufuatiliaji wa miamala ya simu za mkononi (TTMS) kuweza kukokotoa upya tozo ili kuhakikisha kuwa viwango sahihi vinatumika na kuwa ada na kodi zipo sahihi.
Haya yalibainishwa na CAG, Charles Kichere kupitia Ripoti Kuu ya Ukaguzi wa Mifumo ya Tehema kwa mwaka 2021/22 katika eneo la udhibiti katika mifumo tumizi. Alisema ukaguzi wa Mfumo wa TTMS wa TCRA, CAG aligundua tofauti katika viwango vya tozo kwa miamala ya simu baina ya kiwango kilichotumika na kiwango kilichoanishwa kwenye kanuni, ambapo TTMS inachukua ada na ushuru wa miamala ya simu kutoka kwa mifumo ya waendeshaji bila kuhakiki ikiwa ni sahihi kulingana na kanuni.
“Nilibaini tofauti kati ya viwango vya malipo vilivyopo kwenye kanuni na viwango vilivyotozwa kutokana na mfumo wa TTMS kuchukua ada na kodi za miamala ya simu za mkononi kama zinavyotoka kwenye mifumo ya waendeshaji na kutokuwa na udhibiti wa kuthibitisha kuwa mifumo ya waendeshaji inatumia viwango sahihi.
“Upungufu huu unaweza kusababisha malipo ya kodi inayohitajika kuwa ya chini au ya juu.” Kichere alisema ukaguzi pia ulibaini usuluhishi usiotosheleza kwa ushuru wa miamala ya simu unapelekea kutofautiana kati ya ushuru ulioripotiwa katika TTMS na ushuru uliowasilishwa kwa Mamlaka ya Mapato TRA na waendeshaji. “Chanzo cha tofauti hizi kilichangiwa na utaratibu duni wa usuluhishi wa miamalaka.
Hivyo usahihi wa kodi za serikali hauwezi kuhakikishwa.” “Napendekeza TCRA iliimarisha utaratibu wa usluhishi kwa kuzingatia taarifa zilizoripotiwa kwa TRA na waendeshaji. Pia itekeleze usluhishi baina ya mfumo wa TTMS na mfumo wa e-filing wa TRA kwa uthibitishi wenye ufanisi zaidi.”
CAG alisema ukaguzi pia umebaini kutokuwepo kwa ufuatiliaji wa miamala ya simu za mkononi isiyofanikiwa. “Niligundua kuwa ufuatiliaji wa miamala ya simu za mkononi isiyofanikiwa haufanywi katika mfumo wa TTMS. Nilielezwa kuwa muundo wa TTMS haukuzingatia miamala hii sababu haipaswi kuwa na ada zaidi ya gharama za mtandano zinazohusiana na matumizi ya njia ya USSD.”
“Walakini TCRA imepewa jukumu la kufuatilia na kutoa uhakikisho wa mapato kwa huduma za mawasiliano kulingana na kifingu cha 4-(2) (i) na 4-(2) (j) cha Kanuni za Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (TeleTraffic), 2021. Hii ni pamoja na ad azote zinazotozwa na gharama za waendeshaji kwa madhumuni ya uhakikiwa kodi na uwazi wa Serikali.”
Kutokana upungufu huo, CAG Kichere ametoa mapendekezo kwa TCRA kuimarisha mfumo wa TTMS ili kujumuisha ufuatiliaji wa miamala isiyofanikiwa”Rollback Transactions”