CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimetoa miezi mitatu kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mohamed Mchengerwa kufika mkoani Kagera ili kutatua changamoto zinazowakabili Wananchi ikiwemo ujenzi wa soko usiokamilika, ujenzi wa stendi ya kimataifa na kutatua changamoto ya mto kanoni kwa kujenga Kingo zake.
Maagizo hayo yametolewa leo na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Itikadi na Uenezi, Paul Makonda wakati akizungumza kwenye uwanja wa Mayunga mkoani Kagera katika ziara yake ya Kanda ya Ziwa yenye lengo la kusikiliza na kutatua kero za wananchi.
“Waziri Mchengerwa nakupa miezi mitatu uwe umekanyaga kagera, nataka kuona mpango wa ujenzi wa soko, tafuta pesa kokote soko lijengwe, nataka kuona stendi ya kisasa ya kimataifa inajengwa Kagera pamoja na changamoto ya mto wa Kanoni imalizwe kwa kujenga kingo za mto huo.” alisema Makonda.
Makonda akizungumza kwa njia ya simu na Waziri Mchengerwa alisema ameyapokea maelezo hayo na ni utekelezaji wa Ilani ya chama hicho.