Dk Biteko aagiza Williamson Diamond kuanza uzalishaji

WAZIRI  wa  Madini, Dk Doto Biteko ametaka  uongozi wa   Kampuni ya Williamson Diamond  LTD  inayochimba  madini ya almasi iliyopo Mwadui wilayani  Kishapu mkoani Shinyanga  kuanza kazi ya uzalishaji wa madini hayo Julai 15, mwaka huu.

Kauli hiyo imekuja baada ya kampuni hiyo kusitisha uzalishaji takribani miezi sita  tangu bwawa la  maji tope libomoke  na tope kusambaa  kwenye kaya na  mashamba ya watu.

Dk Biteko  aliyasema hayo  jana  baada ya kufanya ziara  ya kutembelea bwawa la maji tope jipya lililochimbwa kuanzia mwezi Machi likiwa na ukubwa wa hekta 57.2 na litakalo dumu kwa muda wa miaka miwili na nusu.

Advertisement

Alisema  uzalishaji  wa almasi uanze tarehe hiyo na kibali watapewa wiki ijayo siku ya Jumanne  kwenye ofisi ya Mhandisi  Mkuu wa Tume ya madini  na kibali cha watu wa  bonde la maji kitashughulikiwa na kuwa hawana sababu ya kushindwa.

“Nina upongeza uongozi wa mgodi huu, serikali ya mkoa na wilaya kwa ushirikiano mzuri mlio uonyesha kwani mlisimama hakuna siasa iliyoingizwa na kila mwananchi aliyeathirika kapata haki yake,” alisema.

Mkaguzi Mkuu kutoka Tume ya Madini, Henry Nditi alimueleza  Biteko  kibali kipo muda wowote watakapohitaji kwani bwawa hilo limeonekana kukamilika kiasi kikubwa.

Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Modest Mkude alisema hakuna mgogoro wowote katika eneo hilo na kwamba hali ni shwari na asilimia 96 ya wanachi walioathirika wamelipwa  fidia.

Mbunge wa Jimbo la Kishapu, Boniface Butondo  alisema anaishukuru serikali kwa kuchukua hatua na kulisimamia suala hilo ambalo limeenda vizuri kwani mgodi huo umesaidia kunyanyua uchumi wananchi  wa wilaya hii kwa kulipa mapato na kutoa ajira.

Meneja Mkuu wa mgodi wa almasi Mwadui, Ayoub  Mwenda alisema wao wako tayari kuanza uzalishaji kuanzia wiki ijayo wanachosubiri ni kibali kutoka ofisi za madini  kwani bwawa hilo limekamilika na mitambo iko vizuri.

Mhandisi kutoka kampuni ya City Engineering Anael Macha ambaye alikuwa akichimba  bwawa hilo alisema lilianza kutengenezwa mwezi  Machi, mwaka huu na sasa limekamilika na litadumu kwa muda wa miaka miwili na nusu na lina ukubwa wa hekta 57.2

4 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *