Dk Biteko aisifu REA utekelezaji miradi

DODOMA: NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko ameupongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kufanya vizuri katika utekelezaji wa majukumu yake ikiwemo usambazaji umeme kwenye vijiji, vitongoji na usimamizi wa miradi ya nishati jadidifu ikiwa ni utekelezaji wa mipango ya Wizara ya Nishati.
Ametoa pongezi hizo jijini Dodoma wakati wa kikao chake na Menejimenti ya Wizara ya Nishati na Taasisi zilizo chini yake ikiwa ni kikao cha pili toka uanzishwe mfumo mpya ndani ya wizara na taasisi zake wa kujifanyia tathmini ili kuona namna inavyofanya kazi ya kuhudumia wananchi.
Katika kikao hicho, ilitolewa tathmini ya utendaji kazi wa taasisi zilizo chini ya wizara iliyofanyika katika kipindi cha miezi mitatu kinachoishia Septemba 2024 ambapo Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imeongoza kwa kufanya vizuri ikifuatiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA).