Dk Mwigulu ahimiza umoja kutekeleza Dira 2050
WAZIRI Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba amehimiza watendaji wa serikali, viongozi na Watanzania kuunganisha nguvu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Dk Mwigulu alisema hayo alipozungumza na wahariri wa vyombo vya habari Dar es Salaam.
Alisema dira hiyo imebeba matarajio ya ustawi wa Watanzania hivyo utekelezaji wa dira hiyo unahitaji umoja, nidhamu na kasi kwa ajili ya kufanikisha mwelekeo mpya wa maendeleo na manufaa ya wananchi.
“Dira hiyo imebeba mambo mengi ya maendeleo ya Watanzania, tunakazi kubwa tukiwa katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ni vizuri wote tukaunganisha nguvu katika jambo hili kubwa, tukichelewa kidogo tutakuwa tumeharibu kasi ya utekelezaji wa dira hii,” alisema Dk Mwigulu.
SOMA: Mwigulu atoa agizo usafiri mwendokasi
Alisema Rais Samia Suluhu Hassan katika hotuba zake ameagiza kasi wanayotakiwa kwenda nayo katika utekelezaji wa masuala ya maendeleo inatakiwa iwe kubwa kuliko ile iliyopita kwa sababu wanaanzisha utekelezaji wa dira hiyo.
“Kile tunachotaka kukifanikisha kwa namba unaweza kukiona ni cha kawaida lakini kwenye uhalisia ni jambo kubwa inahitaji tujifunge mkanda na tuunganishe nguvu na kiuhalisia inahitajika tufanye jitihada kubwa kufikia hapo,” alisema.
Aliongeza kuwa inapaswa Watanzania wote wakaunganisha nguvu katika kushughulikia na asilimia nane ya Watanzania walioko kwenye umaskini wa kupindukia na asilimia 26.4 walioko kwenye umaskini wa kipato.
Mwigulu alisema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka huu kwa mara kwanza ndio imejikita kwenye maisha ya maendeleo na mafanikio ya Mtanzania mmojammoja.
“Ilani ya sasa haizungumzii kufikisha umeme kwenye kijiji inaongelea kuunganisha umeme kwenye kila kaya, inaongelea Watanzania kuhama kutoka kwenye kupikia kuni na mkaa kwenda kwenye nishati safi ya kupikia ifikapo 2030 na kiongozi wa programu hiyo kimataifa ni Rais Samia Suluhu Hassan,” alisema.
Alifafanua kuwa ilani hiyo inazungumzia maendeleo ya Watanzania walioko vijijini, miundombinu wezeshi kwenye ngazi ya uzalishaji katika umwagiliaji, kusafirisha mazao na mengineyo kwa ajili ya maisha bora na maendeleo ya kila Watanzania.
Alisema ili kufanikisha hayo inahitajika Watanzania waunganishe nguvu kwa kushirikiana na watendaji wote wa serikali, mhimili wa sheria na bunge.
“Sisi upande wa serikali tumejipanga kuhakikisha tunatekeleza kwa vitendo maelekezo ya Rais Samia ambayo ndiyo dira ya kwamba tunahitaji tufanye kazi kwa kasi zaidi itatuhitaji tuache kufanya mambo kimazoea,” alisema.
Alieleza kuwa Rais Samia hivi karibuni alibainisha kuwa kutakuwa na uhaba wa rasilimani kwa hiyo lazima watumie kwa uadilifu na ipasavyo rasilimali zilizopo nchini kwa ajili ya maendeleo ya taifa ambapo watafuatilia uadilifu, nidhamu kazini na bidii ya kila mtendaji.
Alisema serikali haitasita kuwachukulia hatua watumishi wake wasiokuwa waadilifu kwa sababu bila nidhamu na uadilifu hawatafanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050.



