Kituo cha Biashara Russia-India Kimeanzishwa

SERIKALI ya India imesema itaendelea kushirikiana na Urusi kuimarisha uhusiano wao wa kibiashara kwa kuanzisha Kituo cha Biashara cha Russia-India (Russian-Indian Trade House), hatua inayochukuliwa kuwa maendeleo makubwa katika ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili.
Makubaliano haya yamesainiwa katika Jukwaa la Viwanda la Urusi 2025, lililofanyika mjini St. Petersburg, chini ya Shirikisho la Vyumba vya Kimataifa vya Biashara (Union of International Trade Houses), ambalo tayari lina matawi katika nchi za Vietnam, Mongolia, China, Cambodia, na Thailand.
Kituo hiki kipya, chenye makao makuu mjini Delhi, kitahimiza biashara ya pande zote mbili, uwekezaji, utalii, kubadilishana teknolojia, na ushirikiano wa wafanyakazi. SOMA: Ethiopia Yaingia BRICS
Mkurugenzi wa Kituo hicho, Prashant Chaudhary, amesema hatua hii itaunda fursa mpya kwa biashara za India na Urusi kushirikiana na kukuza uchumi, huku ikihakikisha mfumo rahisi wa biashara na maendeleo ya ujuzi. Ameongeza kuwa mpango huu utarahisisha mazungumzo, uwekezaji, na kubadilishana teknolojia kwa manufaa ya pande zote mbili.
Rais wa Shirikisho la Vyumba vya Kimataifa vya Biashara, Roman Malinovsky, amesema kuwa kuanzishwa kwa Kituo cha Biashara cha Russia-India kutaimarisha zaidi uhusiano wa kibiashara kati ya India na Urusi na kufungua njia mpya za ushirikiano wa kiuchumi.
Takwimu rasmi zinaonyesha kuwa biashara kati ya India na Urusi mnamo mwaka 2024 ilifikia dola bilioni 70, kiwango cha juu zaidi hadi sasa. Kituo hiki kitasaidia kupanua ushirikiano katika sekta za nishati, viwanda, kilimo, dawa, na huduma, huku kikiunda jukwaa la kudumu la kushirikiana kiuchumi na kiufundi kati ya pande hizo mbili.


