Misri kuwekeza kilimo cha umwagiliaji

SERIKALI ya Tanzania na Misri zimekubaliana kuimarisha ushirikiano katika sekta ya kilimo, hususan kilimo cha umwagiliaji, kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa chakula na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Akizungumza Ikulu, Dar es Salaam, wakati akitoa taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu ziara ya Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Abdel Fattah El-Sisi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan amesema ushirikiano huo unalenga kutumia uzoefu wa Misri katika teknolojia za kilimo cha umwagiliaji ili kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

Dk. Samia amesema kila mwaka nchi za Afrika hutumia kati ya dola za Marekani bilioni 70 hadi 100 kuagiza bidhaa za chakula, zikiwemo mchele, ngano, sukari, mahindi, nyama, maziwa na mafuta ya kula, hali inayoonyesha umuhimu wa kuongeza uzalishaji wa ndani. SOMA: Samia: Tanzania, Misri kuimarisha uchukuzi

“Tanzania ina takribani hekta milioni 29 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Misri imepiga hatua kubwa katika teknolojia za umwagiliaji na uzalishaji wa mbegu kwa kutumia maji ya Mto Nile. Sisi tuna mito, maziwa na mabwawa mengi, lakini bado hatujafikia kiwango kinachostahili katika kilimo cha umwagiliaji. Ndiyo maana tumeamua kushirikiana nao ili kukuza sekta yetu ya kilimo,” alisema Dk. Samia.

 

Ameongeza kuwa, mbali na kilimo cha umwagiliaji, Misri imeonyesha nia ya kuwekeza katika sekta ya mifugo hatua inayotarajiwa kuongeza tija katika uzalishaji wa nyama, maziwa na bidhaa nyingine za mifugo.

Aidha, Rais Samia amesema kwa sasa Misri ni miongoni mwa wawekezaji wakubwa nchini, ikiwa imewekeza katika sekta mbalimbali zikiwemo nishati, kilimo, viwanda, ujenzi na utalii. Amesema thamani ya uwekezaji huo imefikia dola za Marekani bilioni 1.5 na umechangia kutoa ajira kwa zaidi ya Watanzania 4,000.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button