Israel yakataa kujadili sitisho la vita na Hezbollah

WASHINGTON, Marekani — Israel imesema haitajadili sitisho la vita na kundi la Hezbollah wakati wa mazungumzo na maafisa wa Lebanon yatakayofanyika Marekani wiki ijayo.
Balozi wa Israel, Yechiel Leiter, alisema mazungumzo hayo yatakuwa mwanzo wa majadiliano rasmi ya amani kati ya Israel na serikali ya Lebanon, licha ya kutokuwepo kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa Israel haitashiriki majadiliano yoyote yanayohusisha Hezbollah, akilitaja kundi hilo kama kikwazo kikuu cha amani na linaloendelea kufanya mashambulizi dhidi ya Israel.
Hatua hiyo inakuja wakati mashambulizi ya Israel yakiongezeka nchini Lebanon, ambapo vyombo vya habari vya ndani vimeripoti vifo vya watu watatu kufuatia shambulio la anga lililoharibu jengo la makazi katika eneo la Nabatieh.
Wakati huo huo, Marekani na Lebanon zimeripotiwa kuitaka Israel kusitisha mashambulizi kwa muda kabla ya mazungumzo hayo, ili kutoa nafasi ya mafanikio ya kidiplomasia.
Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema amemshauri Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kupunguza mashambulizi, akionya kuwa hali hiyo inaweza kuhatarisha juhudi za sitisho la vita kati ya Marekani na Iran.



