JK aongoza mahafali ya 17 MUCE

IRINGA;Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Rais mstaafu wa Awamu ya Nne Dk Jakaya Kikwete, ameongoza mahafali ya 17 ya Chuo Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE) mjini Iringa leo, ambapo ametunuku shahada mbalimbali za umahiri na za awali kwa wahitimu.
Katika ngazi ya umahiri, amewatunuku Digrii ya Umahiri wa Sayansi na Ualimu (Master of Science with Education) kwa wahitimu wanne, Joyce Dismas, Osia Mwanyesya, Deogras mmanuel na Samwel Lungo.
Aidha, wanafunzi wawili, Mbazi Senkondo na Joseph Luoga—wamepata Digrii ya Umahiri wa Sayansi katika Ubunifu wa Kihisabati (Master of Science in Mathematical Modelling), huku John Ngazime Josephat akitunukiwa Digrii ya Umahiri wa Elimu Jamii na Ualimu (Master of Arts with Education).
Kwa upande wa Shahada za Awali, jumla ya wahitimu 565 wamepata Digrii ya Awali ya Elimu Jamii na Ualimu (Bachelor of Arts with Education). Wahitimu wengine 365 wametunukiwa Digrii ya Elimu katika Sayansi (Bachelor of Education in Science), 334 wakipewa Digrii ya Awali ya Sayansi na Ualimu (Bachelor of Science with Education), na 17 wakitunukiwa Digrii ya Awali ya Sayansi katika Kemia (Bachelor of Science in Chemistry).
Katika kilele cha hafla hiyo, Mkuu wa Chuo amekabidhi pia Cheti cha Ubora kwa mhitimu aliyeng’ara zaidi, Lekishin Koipa, aliyepata ufaulu wa daraja la kwanza kwa wastani wa GPA 4.8—ikiwa ndiyo alama ya juu zaidi miongoni mwa wahitimu wote wa MUCE mwaka 2025.



