DAR ES SALAAM: Waziri wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki amezindua Kamati ya Kitaifa ya kuongoa shoroba za wanyama pori katika kongamano la kwanza la kitaifa la kujadili usimamizi madhubuti wa shoroba hizo ili kuleta manufaa ya kiuchumi huku akiielekeza kamati hiyo kufanya kazi kwa kasi zaidi.
Katika hotuba yake aliyoitoa leo Desemba 14, 2023 jijini Dar es Salaam kwenye kikao cha wadau zaidi ya mia mbili, Kairuki amesisitiza kuwa katika usimamizi huo wizara itashirikiana na wadau mbalimbali ili kufikia azma hiyo kwa kuwa jambo hilo haliwezi kutekelezwa na wizara peke yake na amewaomba wadau wa ndani na nje ya nchi kujitokeza kushirikiana na serikali.
Amesema sambamba na zoezi hilo serikali itaendelea kutekeleza mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo ya shoruba ili maeneo hayo yaweze kutumika kikamilifu katika mawanda mengine kama utalii wa picha hivyo kuinufaisha jamii inayozunguka maeneo hayo na nchi kwa ujumla wake.
Ameongeza kuwa kukamilika kwa matumizi bora ya ardhi pia yatasaidia kuainisha maeneo yatakayotumika kwa ajili ya huduma za kijamii kama shule hospitali, kilimo na malisho.
Amefafanua kuwa pia lengo la kikao cha kwanza cha jukwwa la kitaifa la kuongoa shoroba ni kujadili suala la kuhifadhi shoroba za wanyamapori nchini ili kutekeleza Mpango wa Kuongoa na Kusimamia shoroba 20 za Wanyamapori za Kipaumbele nchini – 2022-2026, (Tanzania Wildlife Corridors Assessment, Prioritization and Action Plan).