Kakele aipa tano TSN

NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Selestine Kakele ameipongeza Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) kwa kuanzisha huduma ya habari mtandao ikiwemo gazeti la mtandaoni (E Paper).
Kakele ametoa pongezi hizo leo Julai 4, 2023 alipotembelea banda la TSN katika Maonesho ya 47 ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba na kujionea huduma mbali mbali zinazotolewa na TSN.
Amesema, “ TSN ni moja ya taasisi zilizoko chini ya Wizara ya Habari, ni taasisi kongwe wizara ni mpya imeanzishwa miaka miwili chini ya mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.” Amesema na kuongeza
“TSN na wazo la E Paper ni mahitaji ya dunia, dunia inaenda kasi katika teknolojia hivyo ipo haja ya kuchakata taarifa ambazo zinazalishwa.
“Ni mwelekeo sahihi, tunawapongeza, tuangalie pia wenzetu waliotutangulia katika eneo hilo changamoto zilizowakumba na kuchukua tahadhari.”Amesema
Amesema, Wizara itaendelea kushirikiana na TSN kuwafikia watanzania katika kuwapasha habari.
Aidha, amesema ujenzi wa Kiwanda cha uchapishajji kitaiongezea nguvu TSN katika uendeshaji na kutatua majawabu ya msingi ya mtaji na uendeshaji kwa ujumla.
“Kama ambavyo wanasema hawatajielekeza tu kuchapisha Magazeti ya Serikali lakini pia watatoa huduma watakaohitaji huduma hiyo watafikiwa na watapata huduma hiyo, hiki ni chanzo cha mapato cha uhakika cha TSN, jambo ambalo ni la msingi na uendelevu kama taasisi.”Amesema.
Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa TSN Tuma Abdallah amewasihi wananchi kutembelea Banda la TSN kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo.