Kampuni kutoa mafunzo afya ya akili mahala pa kazi

MPANGO wa mafunzo ya afya ya akili mahali pa kazi kwa watumishi wa sekta ya umma na binafsi umezinduliwa rasmi ukiwa na lengo la kuboresha huduma za afya ya akili katika maeneo hayo kuhakikisha taifa linakuwa na rasilimali yenye afya bora.

Akizungumza baada ya kuzinduliwa kwa programu hiyo mkoani Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Bloom Wellness Tanzania Ltd, Sophia Byanaku alisema ipo haja ya kujumuisha programu za afya ya akili kwa watumishi mahali pa kazi.

Byanaku ambaye kampuni yake kwa kushirikiana na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) wanatarajiwa kuendesha mafunzo hayo maalumu ya afya ya akili mahali pa kazi, alisema mpango huo ni wa kwanza na wa aina yake nchini.

Advertisement

“Mpango huu wa mafunzo ni wa kwanza wa aina yake hapa nchini unalenga kuwasaidia wafanyakazi kutoka sekta ya umma na binafsi, kuwapa elimu ya afya ya akili na tunashauri mafunzo haya yawe katika mipango mikakati ya kila mwaka ya waajiri kama ilivyo bima ya matibabu,” alisema Sophia.

Katika uzinduzi huo, kundi la kwanza la washiriki wa mafunzo hayo wametoka mashirika tofauti yakiwamo Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Benki ya Amana, Taasisi ya Doctors Plaza Polyclinic, Global Education Link, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (Tasac).

Alisema ushiriki wa watumishi hao ni mwanzo wa juhudi za kitaifa kushughulikia ustawi wa afya ya akili mahala pa kazi.

Alishukuru waliohudhuria mafunzo hayo na kusema yanaboresha ustawi wa afya ya akili hivyo ni vyema taasisi, mashirika na waajiri nchini waone umuhimu wa mafunzo haya kwa waajiriwa wao.

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *