Kampuni yajizatiti kulinda mazingira

DAR ES SALAAM: KAMPUNI ya Africa Global Logistics (AGL) imetekeleza kwa mafanikio mpango wake wa “Plastic-Less” unaolenga kupunguza matumizi ya chupa za plastiki za maji zinazotumika.

Hatua hiyo ni sehemu ya juhudi zake za kulinda mazingira na kuimarisha matumizi endelevu ya rasilimali.

Mpango huo haukulenga kuondoa kabisa matumizi ya plastiki, bali kupunguza utegemezi wake kwa kuhimiza matumizi ya njia mbadala endelevu ndani ya kampuni.

Katika utekelezaji wake, AGL imesambaza chupa za maji zinazoweza kutumika mara kwa mara kwa wafanyakazi wote kwa ajili ya matumizi ya kila siku na mikutano, hatua iliyosaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza matumizi ya chupa za plastiki zinazotupwa baada ya matumizi moja.

Aidha, kampuni imeweka mitambo ya kuchotea maji (water dispensers) katika vyumba vya mikutano pamoja na maeneo ya idara mbalimbali, ili kurahisisha wafanyakazi kujaza maji kwenye chupa zao wakati wowote. Kwa wageni, kampuni imeandaa matumizi ya glasi ambazo husafishwa kwa mashine maalum kuhakikisha viwango vya juu vya usafi vinazingatiwa.

Akizungumza wakati wa utekelezaji wa mpango huo, Meneja wa Sheria wa AGL, Angeline Mtulia, alisema uendelevu ni sehemu ya dhamira ya kampuni na ni jukumu la kila mfanyakazi kushiriki katika kulinda mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

“Kupitia mpango wa ‘Plastic-Less’, tumeonyesha kuwa mabadiliko madogo ya kitabia, yakisaidiwa na miundombinu sahihi na ushirikiano wa kijamii, yanaweza kuleta matokeo makubwa ya kimazingira na kijamii,” alisema Mtulia.

Kampuni hiyo imeeleza kuwa itafuatilia kwa karibu utekelezaji wa mpango huo kupitia idara ya usalama, ambayo itakuwa ikikusanya na kuchambua takwimu za matumizi ya plastiki kabla na baada ya utekelezaji wa mpango huo ili kupima mafanikio yake katika kupunguza taka za plastiki.

Uzinduzi rasmi wa mpango huo ulifanyika Juni 5, sambamba na maadhimisho ya kimataifa ya mazingira chini ya kaulimbiu “Act Now for the Climate”, ambapo wafanyakazi walihudhuria wakiwa na chupa zao za maji zinazoweza kutumika tena. Timu ya QHSE ilitoa maelezo ya kina kuhusu malengo ya mpango huo na namna ya kushiriki kikamilifu.

Katika kuimarisha uelewa, AGL pia ilifanya vipindi vya elimu kuhusu usimamizi wa taka na uhifadhi wa mazingira, ambapo kikundi cha “The Recyclers” kilitoa elimu kuhusu athari za matumizi mabaya ya plastiki na umuhimu wa mabadiliko ya kitabia.

Katika hatua ya uwajibikaji kwa jamii (CSR), AGL kupitia kampuni dada ya EALS ilitembelea Shule ya Sekondari Mabibo, ikiendeleza ushirikiano uliopo baada ya kujenga vyoo na kukarabati maktaba mwaka 2025. Katika ziara hiyo, kampuni ilikabidhi ndoo 12 za taka, vizima moto 27 pamoja na kengele ya tahadhari ya moto.

Wanafunzi walipatiwa elimu ya usimamizi wa taka kwa kutumia ndoo zilizotolewa ambazo zilikuwa zimewekewa alama za kutenganisha taka za chakula, plastiki na taka nyinginezo, hatua iliyosaidia kuongeza uelewa wa utupaji sahihi wa taka.

Aidha, ilibainika kuwa shule hiyo ina ushirikiano wa karibu na mamlaka za zimamoto, ambazo mara kwa mara hutoa mafunzo ya usalama wa moto kwa wanafunzi.

Kwa ujumla, mpango wa “Plastic-Less” umeleta matokeo chanya ndani ya kampuni na katika jamii, huku ukichochea mabadiliko ya tabia kuelekea utunzaji bora wa mazingira na usalama.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button