KCJE kujiimarisha kuleta tija ya korosho

SHIRIKISHO la Vyama vya Ushirikia wa Korosho Tanzania (KCJE) limesema litahakikisha inakuwa taasisi bora, imara na yenye kuleta tija kwa mipango inayojiwekea kwa vyama wanachama pamoja na sekta ya korosho nchini.
Hayo yamejiri wakati wa mkutano mkuu wa nne wa kawaida wa mradi wa vyama vikuu vya ushirika wa korosho mwaka 2025/2026 uliyofanyika katika Manispaa ya Mtwara Mikidnani mkoani Mtwara ulioandaliwa na KCJE.

Mtendaji Mkuu wa KCJE, Mohamed Mwinguku amesema taasisi hiyo ni mpya kwani imesajiliwa mwaka 2022 kwa hiyo inaendelea kujiimarisha zaidi kiutendaji na kutengeneza rasilimali mbalimbali zitakazowezesha taasisi kuwa na mwelekeo wenye tija kwa vyama wanachama.
Lengo la mkutano huo ni pamoja na kupitisha makadirio ya mapato na matumizi kwa mapato ya kawaida na yasiyokuwa ya kawaida pia matumizi ya kawaida na yasiyokuwa ya kawaida kwa ajili ya mwaka wa fedha 2025/2026.

Pia ukamilishaji wa mpango mkakakati wa miaka mitano unaoanzia mwaka 2025 hadi mwaka 2029 wa mradi wa pamoja wa mambo mbalimbali ikiwemo ujenzi wa kiwanda cha kuchakata na kuzalisha viuatilifu vya zao la korosho.
Lengo lingine ni ujenzi wa ofisi ya shirikisho hilo inayojengwa Mtwara mjini pia ununuzi wa magari 30 kwa ajili ya shughuli za usafirishaji zitakazofanywa na kusimamiwa na mradi huo wa pamoja.
‘’Tumetengeneza mwelekeo unaoenda kutambulisha miongozo yote itakayowasaidia katika usimamizi na uendeshaji wa mradi huu ili iwe taasisi bora, imara na yenye kuleta tija kwa mipango inayojiwekea kwa vyama wanachama pamoja na sekta ya korosho nchini,’’amesema Mwinguku.

Ameongeza kuwa:‘’Tumepitisha mpango mzuri kabisa wa matumizi ya viuatilifu, manunuzi ya vifungashio, bidhaa za kidjitali kwa ajili ya kuendelea kuongeza bidhaa za kidjitali zilizopo katika maeneo mbalimbali ya kupimia mazao ya wakulima ili kuendelea kurahisisha usimamizi wa mazao hayo ya wakulima’’
Mkutano huo umehudhuliwa na viongozi wakuu mbalimbali wa tasnia hiyo ya korosho nchini akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Mwenyekiti wa CBT, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Warajisi wasaidizi wa vyama vya ushirika kutoka mikoa minne inayolima zao hilo ikiwemo Mtwara, Lindi, Ruvuma na Pwani.



