Kijana wa kimasai avunja rekodi chuo cha Mkwawa

IRINGA: Kijana wa kimasai, Lekishon Koipa, ameandika historia nyingine katika Chuo Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE) baada ya kuibuka kinara wa ufaulu kwa kupata GPA ya juu kuliko wote chuoni 4.8.

Kijana huyo mhitimu wa digrii ya awali ya elimu jamii na ualimu kwa mwaka 2025, ametangazwa kuwa mfano hai wa ushindi dhidi ya vikwazo na ushahidi kuwa elimu inavuka mipaka ya tamaduni na mazingira.

Akimpongeza kijana huyo kwenye mahafali ya 17 ya chuo hicho, yaliyowatunuku wahitimu 1,625 wa digrii za awali na saba wa digrii za umahiri, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk Jakaya Mrisho Kikwete, alisema:

“Lekishon ametuthibitishia kuwa hakuna lisilowezekana. Kama wazazi wake wasingempa nafasi ya kusoma, huenda leo angekuwa anachunga ng’ombe.”

Heshima yake haikuishia hapo; CRDB Bank imemzawadia Sh milioni 2 pamoja na kompyuta yenye thamani ya Sh milioni 1.5 kwa kutambua juhudi zake.

Msimamizi wa Mtihani (MLAU), Prof Agnes Mwakaje aliitumia siku hiyo kutoa tamko la kimataifa kuhusu ubora wa elimu ya Tanzania.

“Tunautangazia ulimwengu kuwa soko la ajira sasa lina vijana kutoka Mkwawa wenye uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali kwa fikra pevu, ubunifu, na matumizi ya sayansi na teknolojia,” alisema.

Akaongeza kwamba digrii wanazokabidhiwa wahitimu hao si mwisho wa safari, bali ni tiketi ya kuingia kwenye soko la dunia lililojaa ushindani, fursa na changamoto zinazoendelea kubadilika.

Prof Mwakaje aliwahimiza wahitimu kutambua kwamba ujuzi wao haujalenga Tanzania pekee bali unahitajika Afrika na ulimwenguni kote.

Miradi ya utafiti, nafasi za masomo ya juu, ubia wa biashara na ajira sasa vinapita mipaka ya nchi, akiwataka wahitimu wasiogope kuota ndoto kubwa za kimataifa.

Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Balozi Mwanaidi Sinare Maajar, alishukuru wadau waliowezesha mafanikio ya chuo, huku akisifu mchango wa serikali kupitia Bodi ya Mikopo kwa kutimiza ndoto za wahitimu wengi.

Naye Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Bodi ya MUCE, Prof William Anangisye, alitoa wito wa kizazi kipya kutumia elimu kutengeneza ajira, badala ya kutegemea kuajiriwa.

“Jengeni stadi za karne ya 21—mawasiliano, ubunifu, fikra tunduizi, ujuzi wa kidijitali na maadili. Mtakuta fursa zilizo nje ya taaluma zenu, msiziogope,” aliwahimiza.

Alionya matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii, akitaka wahitimu waonyeshe ukomavu wa kitaaluma kwenye kile wanachochapisha mitandaoni.

Rasi wa MUCE, Prof Method Semiono, alitangaza kuwa chuo kinafanya jumla ya miradi 32 ya utafiti, ikiwemo 11 mipya iliyoanzishwa mwaka huu.

Miradi hiyo inalenga kutatua changamoto zinazoikabili jamii moja kwa moja ikiwemo utafiti wa kudhibiti mdudu anayeangamiza nyanya (tuta absoluta), tatizo linaloyakumba mataifa mengi.

Hata hivyo, alieleza changamoto ya ucheleweshaji wa fedha za maendeleo, akisema chuo hicho kinadaiwa zaidi ya Sh bilioni 2.9 na wakandarasi na watoa huduma.

Akielezea jitihada za kuboresha miundombinu ya chuo, Dk Kikwete aliahidi kushiriki katika harambee maalum aliyoagiza iandaliwe na chuo hicho kwa ajili ya kutafuta fedha za maendeleo.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button