Mabaraza vyombo vya habari Afrika kukutana Arusha

DAR ES SALAAM – Mabaraza ya vyombo vya habari kutoka nchi mbalimbali za Afrika yanatarajiwa kukutana jijini Arusha kuanzia Julai 14 hadi 17, 2025 kwa ajili ya Mkutano Mkuu wa kwanza wa Mtandao wa Mabaraza Huru ya Vyombo vya Habari Afrika (NIMCA), utakaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC).

Mkutano huo utajadili masuala muhimu yanayohusu udhibiti wa kujitathmini katika sekta ya habari, usimamizi wa maadili, kupambana na taarifa potofu, na matumizi ya teknolojia ya kidigitali kwa maendeleo endelevu. Kaulimbiu ya mwaka huu ni: “Kuimarisha Udhibiti wa Kujitathmini kwa Maendeleo Endelevu Barani Afrika.”

Wadau wanaotarajiwa kushiriki ni pamoja na waandishi, wahariri, maofisa wa serikali, mashirika ya kiraia, taasisi za elimu, sekta binafsi, na washirika wa maendeleo. Mwenyekiti wa Bodi ya NIMCA, Ernest Sungura kutoka Tanzania, anaongoza maandalizi hayo kwa kushirikiana na Timu ya Ushauri wa Kiufundi ya NIMCA.

Kwa msaada kutoka taasisi kama AU, UNESCO, Ford Foundation, SADC na Open Society Foundations, mkutano huo unalenga kujenga misingi thabiti ya uwajibikaji na uhuru wa vyombo vya habari barani Afrika kwa mujibu wa malengo ya Agenda 2063 na SDGs.

“Mei 23, 2024 katika mji wa kupendeza wa Cape Town, Afrika Kusini, ulianza moja ya ukurasa muhimu katika historia ya vyombo vya habari barani Afrika.

“Mkutano wa kawaida wa Baraza la Vyombo vya Habari Afrika uligeuka kuwa kitu kikubwa zaidi na chenye athari: kuzinduliwa rasmi kwa Network of Independent Media Councils of Africa (NIMCA).

“NIMCA si mtandao wa kawaida wa waandishi wa habari au watangazaji. Ni jibu la bara letu kwa wito wa uraia wa habari unaotegemewa, huru, na wenye maadili. Ni jukwaa lenye matumaini makubwa kujenga na kuhakikisha uhuru wa vyombo vya habari, kutekeleza viwango vya maadili, na kusimamia misingi ya demokrasia barani kote.

“Sasa, baada ya mwaka mmoja, safari hii imepiga hatua nyingine ya kihistoria: Mkutano Mkuu wa NIMCA 2025, utakaofanyika tarehe 14–17 Juni 2025, jijini Arusha, Tanzania, katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC),” imesema taarifa ya Mwenyekiti wa NIMCA, Ernest Sungura.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button