Machinga wampongeza Rais Samia bil 200/- za mikopo

KIGOMA: SHIRIKISHO la Umoja wa Wafanyabiashara Ndogondogo Wamachinga (SHIUMA) limempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa ahadi ya kutenga kiasi cha Sh bilioni 200 kutoa mikopo kwa wafanyabiashara hao.
Mwenyekiti wa Taifa wa SHIUMA, Matondo Masanja amesema hayo katika kongamano la Machinga Kanda ya Magharibi lililofanyika mkoani Kigoma likishirikisha viongozi wa shirikisho hilo kutoka mikoa ya Tabora, Katavi na wenyeji Kigoma.

Matondo alisema kuwa Rais Samia ameona umuhimu wa Machinga kutengeneza ajira lakini pia kukuza uchumi wa nchi na kwamba shirikisho litashirikiana na mamlaka za serikali na wadau mbalimbali kuhakikisha fedha hizo zinawafikia Wamachinga.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa awali Rais Samia alitoa Sh bilioni 48 ambazo zilitolewa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo na sasa ameongeza maradufu na kwamba hilo ni jambo kubwa ambalo halina budi kupongezwa kwa nguvu.

Akizungumza katika kongamano hilo kwa niaba ya Mkuu wa mkoa Kigoma, Balozi Simon Sirro Mkuu wa Wilaya Kigoma, Dk.Rashidi Chuachua alisema kuwa kwa niaba ya serikali Rais Samia anatambua mchango wa wafanyabiashara wadogo wadogo katika mchango wa Taifa na ndiyo sababu ya kuwatambua na kuwaweka kwenye wizara maalum na kuwatengenezea fursa za kibenki ili kuweza kutumia fursa hizo kuimarisha shughuli zao.
Dk.Chuachua alisema kuwa kiasi cha Sh bilioni 200 ambazo Rais Samia ameahidi kuzitoa mikopo kwa wamachinga katika ahadi aliyotoa kwenye uzinduzi wa kampeni kwenye viwanja vya kawe jijini Dar es Salaam ni lazima Machinga wazichangamkie kwa kuwa na vitambulisho vya wajasiliamali ambacho ni moja ya vigezo kwenye upatikanaji wa mikopo hiyo.



