Wananchi Mbulu wapokea mikopo ya 10% na pikipiki

MANYARA: WANANCHI wa Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara wamenufaika na mikopo isiyo na riba ya asilimia 10 ya halmashauri, pamoja na ugawaji pikipiki.
Zoezi hilo limeendeshwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu kwa kushirikiana na Benki ya CRDB, kupitia CRDB Foundation chini ya mpango wa Imbeju.
Mikopo hiyo na pikipiki imetolewa kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, hatua inayolenga kuimarisha uchumi wao.

Akizungumza leo, Oktoba 9, katika makabidhiano, Meneja wa CRDB Kaskazini, Cosmas Sadat amesema benki hiyo ilipokea maombi ya vikundi zaidi 60 yenye thamani ya Sh milioni 233, ambapo baada ya uchambuzi vikundi 20 vilikidhi vigezo.
“Tunataka kuona wananchi wakijitegemea kiuchumi. Imbeju ni mbegu ya maendeleo tunayopanda katika jamii, ili vijana, wanawake na watu wenye ulemavu wawe sehemu ya mabadiliko ya kiuchumi,” amesema Sadat.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Michael Semindu, alisema Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu itaendelea kusimamia urejeshaji wa mikopo hiyo ili iwe endelevu na iwafikie walengwa wengi zaidi.
“Serikali inatambua mchango wa sekta binafsi kama CRDB Foundation katika kujenga uchumi shirikishi. Tutahakikisha mikopo hii inaleta matokeo chanya kwa wananchi,” amesema Semindu.
Baadhi ya wanufaika wa mpango huo walielezea furaha yao baada ya kupokea hundi na pikipiki, wakisema hatua hiyo imewapa matumaini mapya ya kujitegemea na kuboresha maisha yao.

Ibrahimu Bajuta, Mwenyekiti wa Kikundi cha Bodaboda Mbulu, amesema mikopo hiyo imekuwa mkombozi kwa vijana wengi waliokuwa wakitegemea pikipiki za mkataba.
“Mikopo hii imetutoa mbali. Sasa tunaweza kumiliki pikipiki zetu binafsi na kuongeza kipato,” amesema Bajuta.
Naye Marry Joseph, mmoja wa wanachama wa kikundi cha wanawake, alisema fedha walizopata zitasaidia kupanua biashara zao za ufugaji wa kuku na kuongeza uzalishaji.
“Kupitia mkopo huu, tunaweza kuongeza idadi ya kuku na kuboresha kipato cha familia zetu,” amesema Marry.
Kupitia mpango wa Imbeju, CRDB Foundation imeendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwawezesha wananchi kiuchumi, kukuza ajira, na kujenga jamii yenye uthubutu wa kifedha.
Hatua hii inatajwa kuwa mfano bora wa ushirikiano kati ya sekta binafsi na Serikali katika kuleta maendeleo endelevu vijijini na kupunguza umaskini.


