Maxim kutoa fursa kwa madereva

Hatua hiyo ni baada ya kuzindua huduma mpya ya usafiri Dar, Dodoma, Moro

Na Mwandishi Wetu

MADEREVA katika baadhi ya mikoa huenda wakakutana na fursa za ajira zitakazosaidia kuongeza kipato na kujiimarisha kiuchumi baada ya Kampuni ya kimataifa ya usafiri wa mtandaoni, Maxim kuzindua huduma zake katika mikoa ya Dodoma, Mwanza na Morogoro.

Licha ya kutoa fursa za ajira kwa madereva, Maxim inalega pia kuongeza ushindani katika soko la usafiri wa mijini ambalo limeendelea kukua kwa kasi nchini.

Maxim, ambayo ilianzishwa mwaka 2003 na sasa inatoa huduma katika zaidi ya miji 1,000 duniani, inatoa usafiri wa pikipiki, bajaji, magari pamoja na huduma za kusafirisha mizigo, yote kupitia programu ya simu janja.

Akizungumza katika uzinduzi uliofanyika Dodoma, Mkuu wa Maxim mkoa huo, Franklin Foy, alisema kampuni inalenga kuongeza fursa za kiuchumi kupitia ubia na madereva pamoja na kutoa huduma nafuu kwa abiria.

“Hatuko hapa kuongeza chaguo tu. Tupo hapa kuwasaidia madereva kupata kipato cha maana na kurahisisha maisha ya abiria kupitia huduma zetu za kidijitali,” alisema.

Kampuni imeweka nauli za kuanzia Sh 500 katika Mwanza na Morogoro, na Sh 1,000 katika Dodoma kulingana na aina ya usafiri. Kwa Dodoma, nauli zinazotumika ni Sh 1,000 kwa pikipiki, Sh 1,900 kwa bajaji na Sh 3,000 kwa magari.

Franklin Foy alieleza kuwa Maxim inajipambanua kama jukwaa la gharama nafuu, ikidai kuwa nauli zake ziko takribani asilimia 15 chini ya wastani wa soko.

Katika kipindi cha awali, madereva wapya wataruhusiwa kujiwekea asilimia 100 ya mapato yao bila kukatwa kamisheni, kabla kampuni haijapanga iwapo itatoza hadi asilimia 25 kama kanuni za Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) zinavyoruhusu.

Soko la usafiri wa mtandaoni nchini limeendelea kubadilika katika miaka ya karibuni, huku huduma za Uber, Bolt na InDrive zikitawala maeneo mbalimbali ya mijini.

Mwaka 2022, LATRA ilipunguza kiwango cha juu cha kamisheni kutoka asilimia 33 hadi 15, hatua iliyosababisha baadhi ya kampuni kupunguza shughuli. Baadaye, kiwango hicho kilirekebishwa hadi asilimia 25 pamoja na ada ya booking ya hadi asilimia 3 ili kuhakikisha uendelevu wa sekta.

Pia, mkuu huyo wa Maxim alieleza kuwa mbali na bei nafuu, Maxim inaweka mkazo kwenye teknolojia na usalama. Programu yake inawezesha abiria kuomba usafiri, kuona nauli kamili kabla ya safari na kufuatilia mwenendo wa dereva kwa wakati halisi.

“Kampuni pia inatumia huduma ya internet calling kuficha namba za abiria na madereva, pamoja na kuweka kitufe cha SOS kwa dharura. Madereva wa Dodoma pia wamekabidhiwa reflector vest kwa ajili ya usalama barabarani.”

Kuingia kwa Maxim kunatarajiwa kuongeza ushindani katika soko, jambo ambalo linawanufaisha abiria kutokana na urahisi, uhakika wa safari na nafuu ya bei. Hata hivyo, baadhi ya madereva ndani ya sekta hiyo bado wanajadili maslahi na athari za viwango vya kamisheni.

Mkuu huyo wa Maxim Dodoma alieleza pia kwa sasa, Maxim inaendelea kusajili madereva na wamiliki wa pikipiki, bajaji na magari kupitia programu yake ya madereva, huku ikitazama Dodoma, Mwanza na Morogoro kama vituo muhimu katika mkakati wake wa kupanua huduma za usafiri wa kidijitali nchini.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button