Majaliwa ampa maagizo Biteko suala la mafuta

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa

DDODOMA; WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk Dotto Biteko kushughulikia suala la upatikanaji mafuta nchini na likifanyika ndani ya wiki moja na majibu yakapatikana taarifa itatolewa kwa Watanzania.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo bungeni leo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mlalo, Rashid Shangazi wakati wa maswali kwa Waziri Mkuu.

Mbunge huyo alihoji mkakati wa serikali kutokana na sintofahamu ya upatikanaji wa mafuta katika vituo mbalimbali vya kuuza nishati hiyo hivi karibuni, ambapo mafuta ya petrol na disel yamekuwa hayapatikani katika baadhi ya maeneo, lakini bei ikishatangazwa yananza kupatikana, lakini pia alizungumzia suala la bei ya mafuta kubadiika mara kwa mara

Advertisement

Akijibu swali hilo Waziri Mkuu amesema ni kweli kuna changamoto ya upatikanaji mafuta nchini, ambapo baadhi ya vituo maeneo kadhaa vilikuwa havina mafuta na kwamba serikali inafanya jitihada mbalimbali kutatua tatizo hilo kuanzia Wizara ya Nishati na hata Kamati ya Bunge ya Nishati wamekaa mara kadhaa kwa ajili ya jambo hilo.

Hata hivyo amesema kutokana na mabadiliko aliyofanya Rais Samia Suluhu Hassan hivi karibuni kwa kumteua Dk Biteko kuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, ameonekana mara kadhaa Dk Biteko akifanya vikao mbalimbali na wadau wa masuala ya mafuta, hivyo amemuagiza kushughulikia suala hilo na likipatiwa ufumbuzi ndani ya wiki moja taarifa itatolewa.

“Niendelee kumuagiza Naibu Waziri Mkuu kushughulikia hili, muhimu zaidi niashati yenyewe ipatikane nchini, suala la bei tunajua zinabadilika wakati wote. Tuhakikishe kwanza nishati inapatikana katika vituo vyote na wakati wote ili watanzania waweze kunufaika na upatikanaji huu,” amesema Waziri Mkuu na kutaka wadau mbalimbali wahusishwe..

Amesema jambo la muhimu kwanza ni kuhakikisha mafuta yanapatikana nchini na kama litafanyika ndani ya wiki moja majibu yakapatikana itatolewa taarifa kwa Watanznaia.

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *