Ida Odinga aitisha amani kumuenzi Raila

MJANE wa Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya, Raila Odinga, Mama Ida Odinga, amezungumza kwa mara ya kwanza tangu kifo cha mumewe kilichotokea nchini India wiki iliyopita.

Akizungumza katika ibada rasmi ya mazishi iliyofanyika jijini Nairobi, Mama Ida alikumbuka kwa hisia safari yao ya ndoa ya zaidi ya miaka 52, akieleza jinsi walivyokutana mwanzoni mwa miaka ya 1970, wakapendana na kufunga ndoa mwaka 1973.

“Safari yetu ya ndoa haikuwa rahisi. Tulikumbana na changamoto nyingi, hasa alipokuwa kizuizini kama mfungwa wa kisiasa. Hata hivyo, tulijifunza kuzungumza kwa uwazi, kusema ukweli, kusamehe na kusonga mbele,” alisema Mama Ida.

Akimzungumzia marehemu Raila, Mama Ida alisema mumewe alikuwa mzalendo wa kweli aliyeipenda Kenya kwa dhati, na kwamba alihuzunishwa na vitendo vya ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma. “Raila alichukizwa na watu waliokuwa wakifuja mali ya wananchi na wale waliopata utajiri kwa njia za kifisadi. Aliamini katika haki, uadilifu na uwajibikaji,” aliongeza. SOMA: Raila aagwa Kitaifa kwenye ibada maalum

Mama Ida aliwataka Wakenya kuenzi kumbukumbu ya Raila kwa kudumisha amani, umoja na upendo, akisema hayo ndiyo maadili ambayo mumewe aliyatetea maisha yake yote. Raila Odinga, ambaye amehudumu kwa muda mrefu katika siasa za upinzani nchini humo, anatarajiwa kuzikwa Jumapili nyumbani kwake Bondo, Kaunti ya Siaya, magharibi mwa Kenya.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button