KAMPUNI ya Magazeti ya Serikali (TSN) imeendelea kuheshimishwa na waandishi wake baada ya awamu hii mwandishi Sijawa Omary kushinda tuzo maalum ya heshima ya uandishi bora wa habari Mkoa wa Mtwara.
Tuzo hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mwanahamisi Munkunda wakati wa kufunga Jukwaa la Habari na Mawasialiano kwa waandishi wa habari na maafisa habari kutoka wilaya zote za mkoa huo, lililohitimishwa leo Novemba 23, 2023.
Aidha jukwaa hilo lilizinduliwa rasmi Novemba 20, 2023 na Mkuu wa Mkoa huo Kanali Ahmed Abbas.
Munkunda amesema tuzo hizo zimetolewa kwa baadhi ya wanahabari bora wa mkoa huo ambao wanafanya vizuri katika kuhabarisha umma, kutangaza habari za maendeleo kwa ufanisi na uweledi mkubwa.
–
Mkuu wa wilaya huyo ameongeza kuwa miongoni mwa waandishi bora waliopata tuzo hizo ni pamoja na mwakilishi wa gazeti hilo mkoani humo ikiwa ni gazeti pekee ambalo limeonekana limefanya vizuri kwa mwaka huu katika kutoa habari zenye mashiko kwa Wananchi na taifa kwa ujumla.
Pamoja na mwandishi wa habari huyo kupatiwa tuzo hiyo pia serikali mkoani wa Mtwara imekabidhi cheti cha Ofisi ya TSN kwa kutambua mchango mkubwa wa TSN kupitia gazeti la HabariLeo ambalo limekuwa linafanya vizuri mkoani Mtwara kupitia mwakilishi wao huyo.
Jukwaa hilo limefanyika kwa muda siku nne lililoambatana na utoaji wa mafunzo kupitia mada mbalimbali zikiwemo kuwajengea uwezo wanahabari kuandika habari zenye kutatua changamoto kwa wananchi na kuleta majibu chanya kwa serikali.