Putin Kim Jong waanza kutekeleza mkataba wa ulinzi

KOREA KASKAZINI : MKATABA wa ushirikiano wa kimkakati kati ya Korea Kaskazini na Urusi umeanza rasmi kwa mujibu wa shirika la habari la Korea Kaskazini, KCNA.
Taarifa iliyotolewa na shirika hilo alhamisi imesema mkataba huo umeanza kazi baada ya Moscow na Pyongyang kukabidhiana nyaraka za kuidhinishwa siku ya jumatano.
Mkataba huo unauweka ushirikiano wa kijeshi baina ya mataifa hayo mawili kwenye ngazi ya juu zaidi, na unaelezea kwamba zitasaidiana pale mmoja wao anaposhambuliwa.
Waziri wa Ulinzi wa Urusi, Andrey Belousov amesema ushirikiano huo unadhamiria kupunguza athari za vita kwenye eneo la kaskazini mashariki mwa Asia. SOMA: Jeshi la Korea Kaskazini laingia Urusi
Mkataba huo unaanza kazi wakati tayari Korea Kaskazini imetuma maelfu ya wanajeshi nchini Urusi kuisaidia kwenye vita vyake dhidi ya Ukraine, kwa mujibu wa duru za kijasusi za mataifa ya Magharibi.