MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam Amos Makalla, amesema wanawake wana kazi nyingi wanazofanya hivyo kuna haja ya kuwa na mpango kazi wa kuleta mabadiliko chanya kwao, ikiwa ni pamoja na kuwafikia wengi zaidi Ili kuleta tija na mabadiliko ya kiuchumi.
Makalla amesema hayo leo Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa viongozi wa majukwaa ya wanawake mkoani humo na kulitaka Jukwaa la Uwekezaji Wanawake kiuchumi mkoa huo kuratibu suala hilo, Ili kuhakikisha wanawake wanafikia ndoto zao.
Amesema mafunzo yanayotolewa kwa viongozi wanawake wayashushe katika ngazi chini Ili kunufaisha wanawake wengi zaidi kwani wanawake wana vipaji vizuri na wakifanya yaliyo makubwa, hivyo ni vyema kwa jukwaa hilo kuhakikisha wanawaelimisha lipi la kufanya na kwa wakati gani.
” Dhana ya uwezeshaji wanawake kiuchumi iende pamoja na kuwapatia fursa mbalimbali zinazopatikana, Ili kuwakwamua kiuchumi,” amesema Makala na kuongeza kuwa viongozi wa majukwaa wahusishe mamlaka za udhibiti katika kazi za wanawake ikiwa ni pamoja na kuwatia moyo.
Amesema mamlaka hizo za Udhibiti kama Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na mengineyo yahakikishe yanawatia moyo wanawake na kazi zao badala ya kuwakatisha tamaaa kwa kuwa wanafanya kazi kubwa .
Amesema pia uondolewe urasimu wa wakaguzi katika kuwafikia wanawake pamoja na kuwatia moyo.
Amesema wanawake ni jeshi kubwa, wasaidiwe mafunzo ya ujasiriamali na fedha washauriwe pia namna ya kukopa pindi mfumo mpya wa mikopo ya asilimia 10 utakapoanza.
Kwa upande wake, Mwenyekiti Majukwa ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi,Fatma Kange amesema wana kazi kubwa ya kuwatia moyo wanawake, Ili kujernga uchumi endelevu.