SHINYANGA: MKUU wa Mkoa wa Shinyanga Christina Mndeme ameitaka kampuni ya Sinohydro Company Limited iliyopewa kandarasi ya kujenga mradi wa Umeme wa Jua wenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 323 kukamilisha kwa wakati.
Mndeme aliyasema hayo alipokuwa akiongea na wadau pamoja na viongozi kutoka shirika la Umeme (Tanesco) na wananchi waliopisha mradi huo kwenye kijiji cha Ngunga Wilaya ya Kishapu huku akieleza mradi huo utatekelezwa kwa kipindi cha miezi 17.
“Mkandarasi uliyepewa dhamana ya kujenga mradi huu mkubwa ninataka ukamilishwe kwa wakati na kwa kuzingatia muda, viwango, thamani na bajeti tuliyokubaliana ili wananchi waanze kunufaika na uwepo wa mradi huu,” alisema Mndeme.
Mndeme aliwakumbusha Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD group) – Dar es salaam Agency na kuwaeleza serikali inafanya kazi bega kwa bega, itawapatia ushirikiano wakati wote wa utekelezaji wa mradi.
Mndeme alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha mradi huu mkubwa wa umeme hasa kuja kutekelezwa katika kijiji hicho na wananchi wa eneo hilo watanufaika kwa kupata ajira.
Naibu Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo Ufaransa AFD Group Dar es salaam Agency Philippe Micheud alisema wameridhishwa na maandalizi yaliyowekwa katika kutekeleza mradi huo na wamevutiwa na eneo lilotengwa katika utekelezaji wake.
Meneja mradi wa umeme Jua Mhandisi Emmanuel Anderson alisema shirika la Umeme nchini (Tanesco) wamejipanga vema katika kusimamia na kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati na kwa kiwango.