SENSA2022: Bashungwa ataka wananchi kutoa ushirikiano kwa makarani

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Innocent Bashungwa ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa makarani wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 ili kupata takwimu sahihi.
Bashungwa ametoa rai hiyo leo baada ya kuhesabiwa nyumbani kwake katika kijiji cha Ahakishaka, Kata ya Nyabiyonza, Wilaya ya Karagwe, mkoani Kagera.
Pia Waziri Bashungwa amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha msisitizo wa kuhesabiwa ambapo ameamka mapema na kushiriki akiwa kwenye Makazi yake Ikulu ya Chamwino Dodoma.
“Niwapongeze watumishi wote wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa kuendelea kuratibu vyema zoezi hili la sensa lililoanza leo na kuhakikisha zoezi linafanikiwa kwa asilimia 100,”amesema.

Aidha, Bashungwa ametoa kwa Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kila mmoja kuendelea kutimiza wajibu wake kwa kushirikiana na Kamati ya Uratibu wa Sensa ngazi zote ili kuhakikisha sensa inafanikiwa ipasavyo.
“Niwapongeze Watendaji wa Kata na vijiji, Wenyeviti wa vijiji na vitongoji kwa namna wanavyotoa ushirikiano na kusimamia zoezi niwatie moyo kuendelea kufanya kazi hii kwa uadilifu ili kuisaidia Serikali kutimiza malengo ya kupata takwimu sahihi kwa maendeleo ya taifa,”amesema.