SMZ kuongeza bajeti ya elimu tril 1/-

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Hussein Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inakusudia kuongeza bajeti ya sekta ya elimu kufi kia Sh trilioni moja ili sekta hiyo iwe kipaumbele kwa maendeleo ya nchi.
Dk Mwinyi amesema hayo wakati wa ufunguzi wa shule mpya ya msingi ya Muungano ya ghorofa tatu iliyopo Kibanda Maiti, Mkoa wa Mjini Magharibi, ikiwa ni sehemu ya shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 62 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
“Bajeti ya wizara ya elimu nataka katika bajeti ijayo tufikie trilioni moja elimu itaendelea kuwa sekta mama ya huduma za jamii katika serikali na tutaendelea kujenga skuli (shule) za ghorofa kama hii Unguja na Pemba,” alisema. Dk Mwinyi alisema ni wajibu wa serikali kuhakikisha kila mtoto anapata mazingira bora ya kujifunzia, na kulinda misingi ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 ya haki, usawa na upatikanaji wa huduma za msingi ikiwemo elimu.

Amesema Serikali ya Awamu ya Nane tayari imejenga shule 35 za ghorofa, hali iliyosaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani. Dk Mwinyi amesema lengo la serikali ni kuondoa changamoto ya uendeshaji wa shule kwa zamu ya asubuhi na mchana na tayari imesaini mkataba na Benki ya CRDB wa thamani ya Sh bilioni 240 kwa ajili ya ujenzi wa shule 29 za ghorofa.
Amesema maandalizi ya ujenzi wa shule hizo umeshaanza katika maeneo ya Fuoni Kibondeni, Jumbi na Chunga kwa Unguja, na Kiuyu Minungwini, Mchanga Mdogo na Micheweni kwa Pemba kupitia mradi unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.

Sambamba na hilo Dk Mwinyi amesema serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Tehama katika sekta ya elimu, na katika mwaka wa fedha 2025/2026 imepanga kuziunganisha shule 70 na mkongo wa mawasiliano. Amesema serikali pia itatoa kompyuta za mezani 2,000 kwa ajili ya maabara, kompyuta mpakato 4,000 kwenye shule pamoja na kuanzisha Madarasa Janja 25 kwa lengo la kuongeza ufanisi wa ufundishaji na kujifunzia.
Katika kuimarisha rasilimali watu Dk Mwinyi amesema tayari serikali imeajiri walimu 492 katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku lengo likiwa ni kuajiri walimu 1,500 pamoja na kuboresha maslahi yao. SOMA: Dk Mwinyi apokea tuzo kivutio bora Afrika




