UONGOZI wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), umepongezwa kwa kuanzisha utamaduni wa wafanyakazi kushiriki michezo ili kujenga afya zao.
Kauli hiyo ilitolewa na Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya TBS, Rwalib Mmbaga, wakati akifungua mashindano ya michezo mbalimbali yaliyoandaliwa na shirika hilo mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam.
Alisema kwa maendeleo ya teknolojia ambayo dunia imefikia kwa sasa ni wazi kwamba afya za watu ziko hatarini, kwani vyombo vya usafiri vimeongezeka na hata yule ambaye hana gari, anatumia boda boda na hata mtu akitaka fedha kutoka benki, anazipata hapo hapo akiwa nyumbani kupitia simu.
“Ukiwa ofisini kazi nyingi zinafanyika kwa njia ya mtandao, ukitoka ofisini unapanda gari lako na kurudi nyumbani, kwa hiyo muda wa kufanya mazoezi unakuwa mdogo.”

“Ndiyo maana napongeza menejimenti ya TBS kwa kuanzisha utaratibu huu, kwani michezo inajenga afya na kuwafanya wafanyakazi kuwa sehemu ya familia moja,”alisema Mmbaga.
Alishauri michezo hiyo ipanuliwe zaidi kwa kuwashirikisha wafanyakazi wa shirika hilo wanaofanyakazi kwenye kanda mbalimbali nchini.
Alisema anajua kwamba sio rahisi kuwashirikisha wafanyakazi wote, lakini wanaweza kuleta wawakilishi ili kujumuika na wafanyakazi wa makao makuu kushiriki michezo hiyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Yusuf Ngenya, alisema mwaka huu ni mwaka wa tatu michezo hiyo kufanyika lengo likiwa ni kuwaweka karibu wafanyakazi na kujenga afya zao.
“Kwa hiyo hii ni njia mojawapo ya kuwafanya wafanyakazi wafahamiane na kujenga afya zetu, kwani afya ni mtaji muhimu sana katika maisha ya kila siku.”
