TEMBO 500 wanatarajiwa kuhamishwa kutoka kwenye msitu unaozunguka Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera na kupelekwa hifadhi ya Burigi Chato na Hifadhi ya Rumanyika.
Hayo yamesemwa na Mhifadhi Mkuu wa Burigi Chato Ismaily Omary leo Oktoba 4, 2023 jijini Dar es Salaam ambapo amesema tembo waliopo kwenye msitu huo wamekuwa wakivamia makazi ya wananchi na kufanya uharibifu mkubwa.
Amesema, sababu kubwa ya |Tembo kwenda kwenye makazi yao wananchi ni kutokana na njia yao kuzibwa na Kiwanda cha sukari cha Kagera ‘Kagera Sugar’ na Ranchi ya Kitengule.
“Kutokana na kupanuka kwa kiwanda cha Kagera Sugar na Ranchi ya Kitengule maeneo ya Tembo ambayo wangepita yamezibwa hivyo wanashindwa kumove na matokeo yake wanaingia kwenye makazi ya wananchi.”Amesema Ismaily.
Amesema, tembo hao wamekuwa wakivamia maeneo ya wananchi katika vijiji tisa vya wilaya ya Karagwe, Bukoba na Misenyi na kuleta hofu kubwa.
Amesema vijiji ambavyo vinaathirika vitatu ni vya wilaya ya Bukoba, vijijini vinne vya wilaya ya Karagwe na vijiji viwili vya wilaya ya Misenyi.