TRC yaongeza safari, mabehewa

SHIRIKA la Reli Tanzania (TRC) limeongeza safari za treni na kuongeza mabehewa katika safari za reli ya kisasa (SGR), reli ya kati kwenda Mwanza na Kigoma na mikoa ya Kaskazini.

Akizungumza na gazeti la HabariLEO, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Uhusiano wa shirika hilo, Fredy Mwanjala alisema kuwa TRC imeongeza seti ya pili ya treni ya mchongoko (EMU) ambayo seti moja hubeba abiria 583, hivyo ongezeko la seti ya pili linamaanisha wanabebwa abiria 1,116 kwa wakati mmoja.

“Lakini pia katika treni yetu ambayo ina mabehewa 14 tumeongeza mabehewa mawili, sasa treni hiyo itaondoka na mabehewa 16, mabehewa hayo mawili moja linachukua abiria 48 lingine abiria 78,” alieleza.

SOMA: SGR yatengeneza ajira 9,376

Aliongeza kuwa, “tuko tayari pia kuhudumia makundi pale tutakapoona inafaa, kwa mfano watu zaidi ya 100 au 200 wakitaka treni sisi tutaona kama inafaa kuwapa treni maalumu tutawapa treni maalumu.”

Kwa upande wa treni zinazofanya safari zake kutoka Dar es Salaam kwenda mikoa ya Kaskazini (Moshi na Arusha) alisema kwa kawaida treni hufanya safari zake Ijumaa na Jumatatu lakini kwa kipindi hiki cha sikukuu wameongeza treni moja ya Jumamosi ambayo itakuwa ikiondoka saa 4:00 asubuhi.

“Mikoa ya Kanda ya Kati kwa kawaida Dar es Salaam hadi Kigoma huwa tunatembeza treni ya behewa 16 lakini Serikali ya Awamu ya Sita waliipatia TRC fedha kwa ajili ya kukarabati mabehewa manne na mabehewa hayo yote yamekamilika, hivyo kuelekea Krismasi na Mwaka Mpya tutatembeza behewa 20,” alisema.

Alieleza kuwa lengo kubwa ni kuhudumia wananchi wanaoelekea katika eneo hilo kwa ajili ya sikukuu za
mwisho wa mwaka.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button