‘Tumieni lugha rahisi kueleza umuhimu wa bima’

Katibu Mkuu Utumishi Dk Laurean Ndumbaro, amewataka watumishi wa bima nchini kuhakikisha wanatoa elimu kwa lugha rahisi, ili kuwasaidia wananchi kufahamu umuhimu wa bima kujikinga na majanga kwa maendeleo yao.
Ametoa rai hiyo wakati akifungua mkutano wa tatu wa baraza la wafanyakazi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima (TIRA) mkoani Tanga.
Alisema kwa kufanya hivyo wataongeza wigo wa watumiaji wa bima, lakini watasaidia kuongeza mchango wao katika uchumi na pato la Taifa kwa ujumla.
“Malengo ya serikali ni sekta hii ya bima kuwafikia na kuwanufaisha wananchi wote, hivyo kuna umuhimu wa kuwa na bima katika maeneo mbalimbali, badala ya kubaki mijini tu, nendeni mpaka kule vijijini na waelimisheni kwa kutumia lugha na mazingira ya kwao,”alisema Dk Ndumbaro.
Naye Mwenyekiti wa baraza hilo, Dk Baghayo Saqware alisema kuwa kwa miaka sita iliyopita kuanzia 2016/21 soko la bima nchini limekua kwa wastani wa asilimia 7, huku matarajio kwa mwaka huu ni kukua kati ya asilimia 8 hadi 10.
Alisema tayari wamejiwekea malengo ya kuhakikisha wanakuza soko la bima na kuongeza watumiaji wake kutoka idadi ya asilimia 15 iliyopo sasa, hadi kufikia asilimia 50.