Ulega asimamisha kazi watumishi Tanroads

SERIKALI imewasimamisha kazi watumishi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) wanaodaiwa kuhusika na uzembe wa kutoshughulikia tatizo la mizani ya Mikese mkoani Morogoro. Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega alitoa agizo wakati wa ziara ya kikazi ya ukaguzi wa miradi ya dharura (CERC) mkoani humo.
Wakati akiwa njiani Ulega alishuhudia msongamano wa magari na alipofuatilia alielezwa chanzo ni kuharibika kwa mzani. “Watu wanateseka na tunaharibu biashara za watu na uchumi wa nchi yetu kwa sababu foleni ina msongamano huu ni mkubwa kiasi cha kufika katika kijiji cha jirani.
Hii haiwezi kukubalika. Wananchi wanateseka kwa kukaa njiani muda mrefu. Biashara zinadumaa. Sitaki kumuonea mtu nataka majibu nani amesababisha hili na kuchukua hatua kwa haraka,” alisema.
Akiwa Mikese, Ulega amepiga simu kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Aisha Amour na akamuagiza asimamishe wahusika wote wa mzani huo ili kuchunguza tatizo linatokana na nini ili watakaobainika kuhusika wachukuliwe hatua.
“Katibu Mkuu nakuagiza wasimamishe watumishi wote walio kwenye mamlaka yangu mpaka nipate kujua chanzo na sababu ya tatizo hili na nani anayefanya uzembe wa jambo hili,” alisema. SOMA: Bosi Tanroads akagua miundombinu BRT Ubungo- Kimara
Aidha, Ulega amemuagiza Aisha ahakikishe timu ya wataalamu inafika Mikese na kutengeneza mzani huo ili kero hiyo imalizike. Mizani ya Mikese mkoani Morogoro ni miongoni mwa maeneo maarufu kutokana na wingi wa magari yanayopita kwa siku kwenda mikoa tofauti nchini na nje ya nchi.



