Viongozi wa dini Kaskazini wahimiza amani

VIONGOZI wa dini kutoka mikoa ya Kanda ya Kaskazini wamewataka Watanzania kulinda amani ya nchi, hasa taifa linapoelekea katika Uchaguzi Mkuu, wakisisitiza kuwa amani ni nguzo muhimu kwa ustawi wa taifa na maendeleo ya watu wake.

Kauli hiyo imetolewa leo, Oktoba 22, 2025, katika Kongamano la Amani na Uchaguzi lililofanyika mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro, likiongozwa na kaulimbiu isemayo “Kupiga kura ni haki yetu, na amani ya nchi yetu ni wajibu wetu.”

Hatahivyo,viongozi wa dini kutoka mikoa ya Tanga, Arusha, Manyara na Kilimanjaro walisoma maazimio ya pamoja yaliyolenga kudumisha amani na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025. SOMA: Watanzania tusimamie misingi, utu wema kulinda amani ya nchi

Katibu wa BAKWATA Wilaya ya Moshi, Alhaji Awadhi Lema, akisoma maazimio hayo, alisema viongozi wa dini wamekubaliana mambo saba muhimu, ikiwemo:Kuhamasisha wananchi waliojiandikisha kuhakiki majina yao na kujitokeza kupiga kura kwa amani,Kuepuka uchochezi, lugha za matusi na maneno ya kuleta chuki kupitia mitandao ya kijamii na vyombo vya habari.

Maazimio mengine vyombo vya dola  kutumia hekima, busara na uadilifu katika kulinda amani siku ya uchaguzi na kuimarisha ushiriki wa viongozi wa dini katika vyombo vya maamuzi na utungaji wa sheria kadhalika kila mwananchi kuwa na wajibu wa kulinda amani wakati wa kudai haki yake.

Sheikh wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mlewa Shaban, alisema hakuna amani ya kweli bila haki, usalama wa uhai na mali. Alisisitiza kuwa jukumu la kulinda amani si la serikali pekee, bali ni la kila raia.“Kuua mtu mmoja ni sawa na kuondoa amani kwa jamii nzima. Raia mwema ni yule anayejenga amani kwa wengine. Amani hujengwa kwa uvumilivu, uadilifu na kuheshimiana bila kujali tofauti za kidini, kikabila au kisiasa,” alisema Sheikh Mlewa.

Mwanasheria wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Mchungaji Wakili Daniel Swai, aliyemwakilisha Askofu Fredrick Shoo, alisema amani na haki haviwezi kutenganishwa, kwani vinashikamana katika kujenga jamii yenye heshima na mshikamano.

Naye Padri Steven Msami kutoka Kanisa la Anglikana Tanga, alisema:“Amani ni tunda takatifu, na palipo na amani watu hukaa kwa utulivu. Tusiseme amani tu, bali tuseme na uvumilivu, kwani bila uvumilivu hakuna amani.”

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Elinawinga Mariki, amewataka vijana kujitokeza kwa wingi kupiga kura, akisisitiza kuwa vijana wana nafasi kubwa katika kuamua mustakabali wa taifa.

Huku Katibu wa BAKWATA Mkoa wa Arusha, Ally Athuman Nassoro, akiwataka Watanzania wanapaswa kutambua kuwa “amani haina mbadala”, hivyo ni wajibu wa kila mtu kuilinda kila wakati wanapokutana na changamoto.“Tumuombe Mungu atupe uongozi utakaoleta maisha bora kwa Watanzania,” alisema Nassoro.

Katika mkutano huo, viongozi hao waliomba vyombo vya ulinzi na usalama kuepuka kutumia nguvu kupita kiasi wakati wa uchaguzi ili kudumisha amani iliyopo nchini.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button