Wabunge waweka mkazo elimu kukabiliana na ebola

WAJUMBE wa Kamati ya Kudumu ya Bunge inayoshughulika na huduma Huduma na Maendeleo ya Jamii wameitaka Wizara ya Afya kuweka mkazo katika zoezi la kuwaelimisha wananchi hususani waishio maeneo ya mipakani ili waweze kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa EbolaW
Wametoa ushauri huo leo, Jumamosi, ikiwa ni siku moja imepita tangu Rais Samia Suluhu awatake wananchi kuchukua tahadhari ya mlipuko wa ugonjwa wa Ebola
Akizungumza wilayani Bukoba mkoani Kager, mjumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Nanyamba Mkoa Mtwara, Abdallah Chikota amemuunga mkono Rais juu ya kauli yake huku akisisitiza umuhimu wa wizara kuweka mkazo katika elimu kwa umma
“Naunga na Rais Samia Suluhu Hassan kuwataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari zinazotolewa na wataalam wa afya. Wizara ya Afya nayo kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu hatari ya ugonjwa huu ili waendelee kujikinga,” amesema Chikota.
Naye Mbunge wa Jimbo la Buyungu, Aloyce Kamamba ambaye pia na Mjumbe wa kamati hiyo, aliwataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari zinazotolewa na wizara hiyo.
Natambua juhudi kubwa zilizofanywa na Wizara ya Afya, naomba tuendelee sasa kuhimiza elimu iendelee kutolewa maeneo yote nchini jamii ichukue tahadhari zote zinazotakiwa, kama taifa, katika kujikinga na maambukizi,” amesema Kamamba
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Kinga, Kitengo cha Elimu ya Afya kwa Umma, Wizara ya Afya, Dk Amma Kasangala amesema wametumia sherehe za kuhitimisha mbio za mwenge ili kufikia kundi kubwa la wananchi wa Mkoa wa Kagera kwa kutoa elimu ya kujikinga na maambukizi.
Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Dunia hadi kufikia Jumatano, wiki hii, jumla ya watu 39 wameripotiwa kufariki na ugonjwa wa Ebola nchini Uganda huku wengine 20 wakiripotiwa kuwa na maambukizi.
Hata hivyo, watu 14 wamepona ugonjwa huo.
Kwa mujibu wa WHO, mamlaka za Uganda zinaendelea kuwafuatilia watu 660 ambao kwa namna moja ama nyingine walikuwa karibu na wagonjwa hao.