Walipa kodi wazalendo wapongezwa Shinyanga

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Shinyanga imewapongeza na kuwapa zawadi baadhi ya wafanyabiashara ambao wamekuwa wazalendo na waaminifu kwa kulipa kodi vizuri kwa hiyari.

Pongezi hizo zimetolewa leo Desemba 19, 2024 na Mwanasheria  wa TRA kutoka Makao Makuu, Elisha Shigela  kwa niaba ya Kamishna wa Mamlaka hiyo, Yusuph  Mwenda ambapo amesema baadhi ya  wafanyabiashara wamejua kazi yao.

Shigela amesema wameamua kutoa zawadi ili wafanyabiashara  wakuwe na waendelee na biashara zao kuisaidia serikali na hawapo  kwaajili ya kuua biashara.

Advertisement

“Mjenga nchi ni mwananchi hivyo wafanyabiashara baadhi wametekeleza kazi yao  na serikali imethamini michango yao,” amesema  Shigela.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Gilitu Enterprises  Manispaa ya Shinyanga, Gilitu Makula amesema  wameipongeza serikali kwa kuondoa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) katika mafuta ya kupikia kwani ni eneo ambalo lilikuwa likiwapa changamoto na sasa wanalipa kodi vizuri kwa maendeleo ya nchi..

“Ninawapongeza sana TRA kufikisha kilio chetu kwa Rais  kwani zamani nilivyokuwa naaza uzalishaji changamoto ya ulipaji kodi ilikuwepo lakini sasa nalipa vizuri nakujua umuhimu wake napongeza sana kuthamini mchango wangu,”amesema  Makula.

Mkurugenzi wa Kampuni  ya Gaki Investment iliyopo Manispaa ya Shinyanga  Gasper Kileo ameishukuru TRA kwa kujua mchango wake na kuwa mzalendo wa ulipaji kodi vizuri.

Mfanyabiashara kutoka Manispaa ya Shinyanga  Clesensia  Ernest  amesema  wanalipa kodi kwa kutambua umuhimu wake  kwani fedha hizo ndizo zinazojenga miundombinu ya barabara, afya, maji na umeme.