VIJANA na watoto wapatao 600 kutoka katika shule na vyuo mbalimbali mkoani Dar es Salaam, wanatarajiwa kunufaika na elimu kutoka kwa wataalamu wa Urusi ya namna roboti za kisasa zinavyotengenezwa na kutumika.
Hayo yalielezwa jana na mwanaanga kutoka nchini Urusi, Anton Shkaplerov wakati akizungumza na
waandishi wa habari katika nyumba ya kitamaduni ya Urusi mkoani Dar es Salaam na kusema ni nafasi nzuri kwa wanafunzi hao kujifunza kuhusiana na roboti na masuala ya anga.
“Ni vyema watoto na vijana wa Tanzania wakipata elimu hii mapema na kwa upande wa Urusi wanafunziwamekuwa wakijifunza masuala hayo kila wanapopata muda kwa kuwa ni kitu ambacho kina umuhimukwa dunia ya sasa,” alisema.
Mkutano wa utolewaji wa elimu hiyo unatarajiwa kufanyika kwa siku tatu kuanzia kesho hadi Jumatano Oktoba 25, mwaka huu katika nyuma ya utamaduni wa Urusi, Dar es Salaam ambapo mwanaanga huyo atashirikiana na vyuo mbalimbali kutoka Urusi.
Shkaplerov aliongeza kuwa jukwaa hilo litakuwa ni fursa kwa Watanzania kupata ufahamu wa namna ya kutumia teknolojia kujinufaisha.
Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya miradi ya Kimataifa kutoka Chuo Kikuu cha Southwest State ambacho ni moja ya chuo kinachoratibu mkutano huo alisema kuwa kupitia wanachokifanya katika baadhi ya nchi wanafunzi wameweza kubuni satelaiti ambazo wataweza kuwaonesha wanafunzi katika mkutano unaoanza kesho ili waweze kujifunza.
“Kuna mfano wa vyuo vya Ecuador ambapo walifanikiwa kubuni satelaiti tatu na zimeweza kwenda
angani, hivyo siku ya pili ya programu yetu tutawaonesha watakaohudhuria ili wajifunze kupitia walichofanya wengine,” alisema.