MKE wa Waziri Mkuu msaafu, Jaji Joseph Warioba, Evelyne Warioba, amewataka wanawake wanataaluma kumuomba Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Taifa.
Amesema ufumbuzi unapatikana kwa Mungu na viongozi wanawake waangalie la kufanya, ikiwemo matatizo makubwa yanayowakumba wanawake na watoto.
Ametoa kauli hiyo Dar es Salaam leo, katika maombi maalum ya wanawake wanataaluma yaliloandaliwa na asasi isiyo ya kiserikali ya uwezeshaji wanawake na vijana kufikia malengo (YLPT), ili kuombea Taifa katika matukio mbalimbali.
Kuhusu wanawake wanataaluma, amesema matatizo makubwa ya vijana vyanzo vyake ni kwenye jamii na wanawake wanataaluma wana mchango wa kunyanyua vipaji vilivyo ndani ya kundi hilo.
Mama Warioba amesema ni wajibu wa wanawake wanataaluma kuomba kwa Mungu kwa ajili ya nchi na viongozi waliomo, ili mipango na mikakati inayopangwa iwe na mafanikio kwa jamii.
“Mara nyingi hatutaki kutumia kile tulichopewa na Mungu kwa ajili ya wengine, labda kwa kuona aibu kwa utaalam tulionao ni vyema kuamka sasa, jambo litakalosaidia kuponya kuanzia ngazi ya familia,” amesema Mama Warioba.
Naye Mkurugenzi wa YLPT, Grace Masalakulangwa, amesema miongoni wanataaluma hao wanaomba kwa Mungu ni pamoja na tathmini ya sensa kuwa na majibu chanya, kuombea serikali na mihimili yake mikuu pamoja na vijana na wanawake waweze kutimiza malengo yao.
Amesema wanawake wanataaluma wanayo nafasi kubwa kurudisha kile walichokipata katika elimu na utumishi pia na kupitia maombi, watasaidia jamii kwa namna moja hadi nyingine.
Amesema kuna haja ya kuombea majibu ya sensa, ili wanaofanya kazi hiyo waifanye kwa weledi, jambo litakalosaidia nchi kufikia malengo ya maendeleo.
” Ni muhimu kwa wanawake wanataaluma kuomba kwa ajili ya Taifa, ili popote wanawake walipo kwenye utumishi na hata katika biashara kutumia taaluma zao kwa uadilifu na kuisaidia nchi kwa namna moja hadi nyingine,” amesema.