Watakiwa kusambaza teknolojia uchakataji mafuta mawese

KIGOMA; TAASISI ya Utafiti wa Kilimo (TARI), kituo cha Kihinga mkoani Kigoma, imetakiwa kusambaza teknolojia ya uchakataji mafuta ya mawese kufikia viwango vya ubora unaokubalika, ili kuhakikisha mkakati wa kuongeza uzalishaji wa mafuta ya kula nchini unafanikiwa.
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Alexander Mnyeti, alitoa agizo hilo wakati akitembelea mabanda na kuzindua maadhimsho ya siku ya chakula duniani, ambayo kitaifa yanafanyika mjini yakitarajia kufikia kilele leo Oktoba 16.
Mnyeti alisema kuwa wakati huu ambapo wakulima wamehamasika kulima zao la michikichi kwa wingi ni vizuri mpango huo ukaenda sambamba na usambazaji wa teknolojia ya uchakati, ambayo itafanya mafuta yanayozalishwa na wakulima wadogo kuwa na ubora, hivyo kufanya lengo la kuongeza uzalishaji wa mafuta ya kula nchini kufanikiwa kwa haraka.
Akitoa maelezo kwa Naibu Waziri, Mtafiti wa kilimo kutoka kituo cha TARI Kihinga, Basil Kavishe alisema kuwa baada ya serikali kuwekeza nguvu kubwa kwenye kuinua kilimo cha michikichi mkoani Kigoma kumeanza kuwa na mafanikio katika kuongeza uzalishaji na sasa mpango ni kusimamia ukamuaji unaozingatia viwango vya ubora.
Kavishe alisema kuwa kwa hatua za awali tayari yupo mwekezaji, ambaye amehamasika na kufungua mashine ya kusafisha mafuta na kuwa na ubora wa juu sambamba na kurudisha virutubisho vilivyopotea.



