Watakiwa kutoa mapendekezo yenye tija usimamizi maafa

MKURUGENZI wa Idara ya Menejimenti ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amewataka wadau wa usimamizi wa maafa nchini kutoa mapendekezo yenye tija katika usimamizi wa maafa ili kukabiliana na kupunguza athari za maafa.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Wadau wa Usimamizi wa Maafa Oktoba 12, 2025 jijini Mbeya, Ndagala amewataka washiriki wa kongamano hilo kuhakikisha wanaibua hoja zenye tija katika kuboresha usimamizi wa maafa.

“Kongamano hili limekusudiwa kuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto, na kutoa mapendekezo ya kuboresha mifumo ya kitaifa ya usimamizi wa maafa,” amesema.

Amesisitiza: “Nitoe wito kwa washiriki wote kushiriki kikamilifu katika mijadala, kwa sababu michango yenu ni muhimu katika kuhakikisha tunapata mapendekezo yatakayokuwa na tija katika usimamizi wa maafa.”

Ndagala amewashukuru wadau wote wanaoendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu katika juhudi za kujenga Taifa lenye ustahimilivu dhidi ya majanga na kuongeza kuwa mchango wao katika kupanga, kutekeleza, na kufuatilia mipango ya usimamizi wa maafa nchini umeendelea kuwa wa thamani kubwa.

Kwa upande wake, Inspector Damian Muheya wa Makao Makuu ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji amesema ili kufanikisha ustahimilivu endelevu usio na maafa, ni muhimu jamii kushiriki kikamilifu katika hatua za kinga na tahadhari dhidi ya majanga.

Naye Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) Dk Barnabas Msongaleli ameeleza kuwa Taasisi yao imeendelea kutoa mchango katika kuzalisha wataalamu wa kada ya usimamizi wa maafa nchini ili kuwa na wabobezi wa eneo hilo na kuendelea kuleta tija katika masuala ya usimamizi wa maafa.

“UDOM tumeendelea kutoa elimu, tunaendesha shahada ya awali ya menejimenti ya vihatarishi vya maafa (Bachelor of Disaster Risk Management). Pia tunafanya tafiti mbalimbali zinazohusu kupunguza au kuzuia vihatarishi vya maafa. Na kutoa huduma kwa jamii kwa njia ya kuwafikia na kuwapa elimu ya vihatarishi vya maafa na namna bora ya kukabiliana na maafa kabla hayajatokea,” amesema Msongaleli.

Vilevile aliwataka washiriki kutumia fursa hiyo kuimarisha ushirikiano na kubuni njia mpya za kuongeza ustahimilivu wa jamii zetu ili kupunguza athari za maafa na kulinda maisha na mali.

Kongamano hilo ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Athari za Maafa kwa mwaka 2025.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button