Waziri Kijaji aitaka Tanapa kuongeza ubunifu

MOROGORO: WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dk Ashatu Kijaji ameagiza Uongozi wa Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuongeza ubunifu wa hali ya juu ili kuchangia kwa kasi kufikia malengo ya Serikali ya kuongeza idadi ya watalii hadi kufikia milioni 8 ifikapo mwaka 2030.

Dk Kijaji ametoa wito huo jijini Morogoro alipotembelea Hifadhi ya Taifa ya Mikumi katika ziara ya kikazi kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika hifadhi hiyo pamoja ba kukutana na Menejimenti ya TANAPA.
Amesema ili kufikia lengo hilo kunahitaji ubunifu, jitihada za kutangaza utalii wa Tanzania kimataifa, ili kuunga mkono maono ya Rais Samia Suluhu Hassan, kupitia filamu za The Tanzania Royal Tour na Amazing Tanzania.

“Tunahitaji ubunifu ndani ya hifadhi zetu zote 21. Kila mmoja wetu atafute kitu cha tofauti ili mtalii apate sababu ya kurudi tena Tanzania, tuibue bidhaa mpya za utalii kila mwaka,” amesisitiza Waziri Kijaji.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Hamad Hassan Chande, amesema licha ya mafanikio makubwa yaliyopatikana katika uhifadhi na utalii, bado ipo haja ya kuongeza kasi ya kutangaza vivutio vilivyopo nchini ili kuongeza mapato kupitia utalii wa ndani.

“Mambo mazuri tuliyonayo tuyatangaze. Neema hii tuliyopewa na Mwenyezi Mungu haipo kila mahali,”.



