Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amewataka watoa huduma katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwananyamala kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na maadili ya kitabibu katika kuwahudumia wananchi pamoja na kuboresha huduma.
Ummy amesema hayo leo Desemba 29, 2022 alipofanya ziara ya kushtukiza katika hospitali hiyo na kukagua utoaji wa huduma, kusikiliza, kero, ushauri na maoni ya wananchi wanaopata huduma za matibabu.
Waziri Ummy ametumia nafasi hiyo pia kutoa elimu ya Bima ya Afya na kuwaasa wananchi kujiunga na skimu mbalimbali za Bima ya Afya kabla ya kuugua ili kuwa na uhakika wa matibabu endapo wataugua.
Aidha waziri huyo amewapongeza watoa huduma kwa kuwa mstari wa mbele katika kuokoa maisha ya watu kupitia utoaji wa huduma bora za matibabu na kuwaasa waendelee kufanya kazi kwa juhudi na maarifa zaidi.