Zaidi ya watu mil 600 hawana umeme Afrika

DAR ES SALAAM: ZAIDI ya Watu milioni 600 Kusini mwa Jangwa la Sahara bado hawajafikiwa na nishati ya umeme.
Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa katika mkutano wa wahariri, wanahabari 175 kuelekea Mkutano wa Nishati wa Wakuu wa Nchi za Afrika ambao Tanzania ni mwenyeji wa mkutano huo unaotarajiwa kufanyika Januari 27-28 mwaka huu.
“Januari 27 ni maalum kwaajili ya Mawaziri wa Nishati wa Afrika kwaajili ya kujadili kuelekea Januari 28 ambao ndio Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika wenye lengo la kuhakikisha watu milioni 300 Afrika wanafikiwa na nishati ya umeme kufikia 2030,” amesema Msigwa.
“Watu milioni 675 bado hawajafikiwa na umeme kati ya watu zaidi ya bilioni barani Afrika,
“Matokeo ya mkutano huo ni kusainiwa kwa Awamu ya Kwanza ya Azimio la Mipango ya Kitaifa ya Nishati kwa kipindi cha miaka mitano 2025-2030,” amesema.
Takribani nchi 14 Afrika zinatarajiwa kunufaika na mpango huo zikiwemo, Mali, DRC, Ivory Coast, Burkina Faso, Madagascar, Chad, Malawi, Nigeria, Mauritania, Niger, Msumbiji, Liberia, Senegal na Tanzania,”
Msigwa amesema, ni fahari kwa nchi yetu kuwa mwenyeji wa mkutano huu ambao mataifa yamevutiwa na juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan kwakuwa kinara wa Nishati Safi ya Kupikia pia kuimarisha usambazaji wa umeme vijijini na vitongojini.



